KLABU ya Azam FC, imemtambulisha mchezaji mpya, Mpiana Mozizi kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
Mozizi aliyekuwa akicheza FC Lupopo aliwasili juzi na kufanya vipimo vya afya jana na endapo atafuzu vipimo vya afya atasaini mkataba wa mwaka mmoja kuitumikia timu hiyo.
Mozizi anayecheza nafasi ya ushambuliaji anakuwa mchezaji wa kwanza kusajiliwa na Azam katika kipindi hiki cha dirisha dogo.
Akizungumza Dar es Salaam juzi, Ofisa Habari wa Azam, Thabit Zakaria alisema mchezaji huyo akifuzu vipimo atasaini mkataba wa mwaka mmoja kuziba nafasi ya Thiery Akono, Novatus Dismas na Shaban Chilunda waliouzwa.
“Baada ya kuwauza wachezaji watatu Novatus, Chilunda na Akono, leo (juzi) tumemsajili mchezaji kutoka FC Lupopo ya Lubumbashi DR Congo kuziba nafasi iliyoachwa na wachezaji waliouzwa hapo awali,” alisema Zakari.
Alisema kama atafuzu vipimo ataanza kuonekana kwenye mchezo wa Kombe la Azam Federation Cup dhidi ya Magereza FC utakaochezwa Disemba 27 Uwanja wa Azam Complex.
Azam ipo kwenye mpango wa kuimarisha kikosi chake kwa ajili ya michezo ya Ligi Kuu Tanzania Bara baada ya kuwa na mwenendo mbaya huku ikishika nafasi ya tatu kwenye msimamo wakiwa na pointi 29 katika michezo 16.