By THOBIAS SEBASTIAN MATAJIRI wa Ligi Kuu Bara Azam FC, msimu huu wameonekana kuanza vizuri baada ya kushinda michezo yao saba ya mwanzo, huku wakiwa wamefunga mabao 14 na wao kufungwa mawili jambo ambalo limepelekea kuvunja rekodi yao ya msimu wa 2015-16, walipocheza mechi sita za mwanzo bila kupoteza na mechi ya saba walitoka sare ya bao 1-1 na Yanga.
Msimu uliopita Azam ilimaliza nafasi ya pili kwenye ligi ikiwa na pointi 63, lakini msimu huu imeonekana kuimarika katika maeneo mengi kuanzia katika usajili ikiwanasa wachezaji wenye mchango kama, David Kissu, Ayub Lyanga na wengineo.
Ubora huo imeonyesha Azam hadi sasa inaweza kuwa miongoni mwa timu ambayo inaweza kushindania ubingwa ambao kwa misimu mingi Simba na Yanga ndio zimekuwa zikitawala kwa kubadilishana kutwaa taji hilo.
Mbali ya kasi hiyo ambayo imeanza nayo msimu huu kuna baadhi ya mambo Mwanaspoti inakuletea kama ikiyashinda inaweza kufikia lengo lao la kutwaa ubingwa lakini wakishindwa kuyashinda halitakuwa jambo la kushangaza kwa mbio zao kuishia ukingoni.
VITA SIMBA, YANGA 2008-09, Azam
Ulikuwa msimu wao wa kwanza kucheza Ligi Kuu Bara na ilianza vizuri mzunguko wa kwanza na kwani mpaka inakwenda mapumziko kwa ajili ya mzunguko wa pili ilikuwa inaongoza msimamo.