Bila kiungo wao nyota, Feisal Salum anayetajwa kutimkia Azam FC, Timu ya Yanga imeibuka na ushindi wa mabao 3-2 mbele ya matajiri wa Jiji Azam FC.
Mchezo huo uliopigwa katika Uwanja wa Benjamin Mkapa Jijini Dar es Salaam, ulikuwa wa kuvutia huku kila timu ikishambulia kwa nguvu kusaka alama tatu.
Walikuwa wenyeji Azam FC kutangulia kupata bao kupitia kwa nyota Abdul Seleman Sopu aliewapa Azam bao la uongozi dakika ya 27 kabla ya Yanga kupata mabao ya haraka kupitia kwa Mayele dakika ya 31 na Aziz Ki akipachika bao safi dakika ya 33.
Mpaka kipindi cha kwanza kinakamilika Yanga walikuwa mbele kwa uongozi wa mabao 2-1.
Kipindi cha pili Azam walirudi kwa kasi na Sopu kwa mara nyingine akawarudisha mchezoni kwa kupachika bao la pili na kufanya matokeo kuwa 2-2.
Farid Mussa akawahakikishia Wananchi kuondoka na alama tatu baada ya kuwaandikia Yanga bao la tatu na la ushindi akimaliza mpira uliotemwa na mlinda lango Ali Ahmada.
Kwa ushindi huo Yanga wanafikisha alama 47 baada ya michezo 18 na kuendelea kujichimbia kileleni mwa msimamo wa Ligi, huku Azam wakibaki nafasi ya tatu na alama zao 37 baada ya michezo 18.