Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Awesu, Kagoma waiponza Simba

Awesu Kagoma 055 Awesu, Kagoma waiponza Simba

Sat, 10 Aug 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Achana na lile sakata la usajili wa beki Lameck Lawi aliyekuwa Coastal Union aliyetimkia kwa sasa KAA Gent ya Ubelgiji, inaelezwa nyota watatu wapya waliosajiliwa na Simba, Awesu Awesu, Yusuf Kagoma na Valentino Mashaka umewaponza Wekundu wa Msimbazi na kuburuza Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).

Wachezaji hao kutoka KMC, Singida Fountain Gate na Geita Gold, wamewekewa pingamizi na klabu tofauti kiasi cha kuifanya Simba kushindwa kuwatumia katika pambano la Ngao ya Jamii lililopigwa juzi kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa dhidi ya Yanga na kulala kwa bao 1-0 lililofungwa na Maxi Nzengeli.

Mwanaspoti limepenyezewa taarifa kwamba Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji ya TFF, inakutana leo Jumamosi kujadili mashauri yaliyowasilishwa kwenye kamati hiyo ikiwamo sakata la Kagoma na Awesu.

Kagoma anatajwa kusajiliwa Simba, huku Yanga ikipeleka pingamizi kwamba hawajarudishiwa pesa zao walizoilipa Singida FG (sasa Fountaine Gate) ili kunasa saini ya kiungo huyo.

Chanzo cha kuaminika kutoka kwa rafiki wa karibu wa Kagoma kimeliambia Mwanaspoti, Yanga walilipa fedha za kumnasa Kagoma kwa klabu husika, lakini ilishindwana na mchezaji aliyekuwa amekubaliana na Simba kuingia mkataba wa miaka miwili.

"Yanga ndio wamepeleka pingamizi la kushinikiza kuwa Kagoma ni mchezaji wao kutokana na kutoa fedha kwa timu iliyokuwa inammiliki na mara baada ya kumalizana na Simba imeshindwa kurejesha kiasi cha fedha walichochukua kutoka Jangwani," kilisema chanzo hicho.

Kwa ishu ya Awesu inaelezwa alishakuwa kwenye mipango ya kocha Fadlu Davids kwa ajili ya mechi ya juzi ya Ngao ya Jamii, lakini Simba ilipokea taarifa kutoka Bodi ya Ligi kwamba hairuhusiwi kumtumia kutokana na kulalamikiwa na klabu aliyokuwa akiichezea ya KMC.

Mwanaspoti ilipata taarifa kwamba, kiungo huyo bado ana mkataba wa mwaka mmoja na KMC ndio maana aliondolewa kwenye mchezo huo baada ya leseni yake kutokupatikana na mabosi wa klabu hiyo waliamua kukimbilia TFF kufungua kesi dhidi yake na Simba.

Ofisa Mtendaji Mkuu wa KMC, Daniel Mwakasungura alipotafuitwa jana alisema ni kweli wamemshtaki Awesu na Simba kwa TFF kwa kukiuka taratibu za usajili kesi hiyo itasikilizwa leo Jumamosi. "Hii haikuwa sawa kabisa walimsajili mchezaji bila kufuata utaribu hivyo na sisi tunakwenda kwenye vyombo vya sheria ili kufikia muafaka wa hilim" alisema Mwakasungura. Hata hivyo, taarifa zaidi kutoka ndani ya klabu ya KMC zinasema kuwa, mkataba wa Awesu ulitakiwa kuvunjwa kwa Sh 50 milioni 50 ambazo mchezaji huyo aliwaingizia kupitia akaunti yao, lakini klabu ilikuwa inataka ilipwe Sh 70 Milioni, hivyo kuamua kurudisha kiasi hicho."

Kwa kesi ya Valentino Mashaka kutoka Geita nae mashtaka yake yanafanana na Awesu na tayari Geita imeshapeleka kesi TFF. Mwanaspoti lilimtafuta Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Said Soud alisema ni kweli leo watakuwa na kikao cha kujadili mashauri yaliyowasilishwa katika kamati hiyo, huku akisisitiza hajui ni mashauri gani yaliyopo hadi watakapokutana ndio atakuwa na nafasi ya kufahamu ni kesi gani zipo mezani kwao. "Kikao kitafanyika kesho (leo), lakini siwezi kuthibitisha ni kesi gani zipo mezani kwasababu huwa tunakutana nazo siku ya tukio kuhusiana na kikao cha leo ni cha mwisho kabla ya dirisha la usajili halijafungwa Agosti 15 mwaka huu," alisema Soud na kuongeza; "Kamati yetu ni sawa na wanasheria mahakamani kesi ambazo hawajawahi kuzisimamia wanakutana nazo maakamani tofauti na zile ambazo zimeshasikilizwa na kupangiwa tarehe nyingine." Soud alisema wanakutana kujadili ni utaratibu wao kukutana mara baada ya usajili wote kukamilika ili kupitia pingamizi zilizopo baada ya usajili.“Dosari kwenye suala la usajili huwa hazikosekani,” alisema. Kamati hiyo pia ilishapitia kesi ya Coastal Union dhidi ya Simba kwa beki Lameck Lawi, ambayo hata hivyo hukumu yake haijatolewa hadi sasa, licha ya beki huyo kutotambulishwa na Simba karuika Simba Day na wiki kadhaa sasa yupo Ubelgiji akijifua na KAA Gent.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live