Ikiwa imebaki saa mbili kabla ya mchezo wa raundi ya 14 kati ya Tanzania Prisons dhidi ya Yanga kuanza, tayari mashabiki wameitika katika Uwanja wa Sokoine huku shabiki Ally Benard akija na zawadi kwa Kiungo Khalidi Aucho
Shabiki huyo wa Yanga ametokea kijiji cha Ilemba wilayani Sumbawanga mkoani Rukwa na leo Februari 11 amewateka mashabiki wenzake baada ya kutinga uwanjani na Jogoo akieleza kuwa ni zawadi kwa kiungo wa timu hiyo, Aucho.
Benard amesema aliwasili Mbeya tangu juzi akiwa na kuku huyo ambaye alimfuga makusudi kwa ajili ya kumtoa zawadi kwa Aucho kutokana na kazi nzuri anayoifanya uwanjani kudhibiti hatari za wapinzani.
Amesema mara kadhaa ameona zawadi nyingi zikiwaendea washambuliaji lakini kwake ameona mchango mkubwa upo kwa nyota huyo wa kimataifa raia wa Uganda ili aamue kama atamchinja au kumpeleka kwao kumfuga.
"Lakini natamani kuonana na Aucho, hii ni zawadi yake maalumu kwa kazi anayoifanya uwanjani, siyo kila siku tunaona wanapewa straika" amesema shabiki huyo.