Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Aucho kukosekana kwenye tuzo za TFF, ugomvi watajwa

Aucho Tuzooo Aucho kukosekana kwenye tuzo za TFF, ugomvi watajwa

Thu, 1 Aug 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Shirikisho la soka Tanzania TFF limetoa orodha ya wanaowania tuzo za msimu wa 2023/24, zitakazotolewa Usiku wa Leo Agosti Mosi kwenye ukumbi wa The Super Dome, Masaki Dar es Salaam.

Katika orodha ya majina yaliyotajwa kuwania tuzo, kuna majina kadhaa ambayo wengi waliamini yalistahili kuwepo lakini hayakuwepo.

Lakini zaidi ya wengi kuamini hivyo, kuna wachezaji nao wanaamini kwamba walistahili kuwania tuzo hizo na wakatoka hadharani na kulalamika.

Mmoja wa wachezaji hao ni Khalid Aucho wa Yanga, aliyeelezea hisia kutokana na kutokuwemo kwenye orodha hiyo, kupitia ukurasa wake wa Instagram. Aucho anasema “There’s no award better than your love and Support. My dear fans thanks always for supporting me from day one. Asante sana”.

“Hakuna tuzo iliyo nzuri kuliko upendo na sapoti. Mashabiki wangu wapendwa daima nawashukuru kwa kunisapoti kuanzia siku ya kwanza. Asanteni sana”

Kauli hii moja kwa moja ililenga kulaumu yeye binafsi kutokuwemo kwenye kuwania tuzo akiamini alikuwa na msimu bora sana ambao ungemfanya astahili.

Ni ukweli usiopingika kwamba kweli Aucho alikuwa na msimu mzuri tangu amekuja Tanzania na msimu uliokuwa bora sana kwake kutokana na uwezo wake mkubwa uwanjani.

Lakini hata hivyo, tuzo zinahusisha vitu vingi sana ikiwemo nidhamu, kitu ambacho Aucho hana. Khalid Aucho licha ya uwezo wake mkubwa dimbani, lakini ni mchezaji mwenye rekodi kubwa ya utovu wa nidhamu uwanjani.

Amekuwa na matukio mengi ya ukorofi uwanjani na ambayo mengi huwa siyo ya kimpira. Kwa mfano tukio lake la Tanga dhidi ya Coastal Union, Novemba 8, 2023.

Aucho alimpiga kiwiko Ibrahim Ajib lakini mwamuzi hakuhukumu ilivyostahili na kumuacha dimbani. Lakini baadaye mamlaka zikajiridhisha kwamba alitakiwa adhabu zaidi, na ndipo ikamfungia mechi tatu zaidi na kumpiga faini ya shilingi laki tano (500,000).

Tukio lile pekee linatosha kumtoa Aucho kwenye kinyang’anyiro cha kuwania tuzo yoyote ya msimu, lakini bahati mbaya kwake anayo mengi yanayofanana na lile. Nidhamu ni kitu muhimu sana kwenye maendeleo ya mchezo huu mzuri na kutoa tuzo kwa watu wenye matukio kama ya Aucho ni kuyahalalisha na kutoa picha mbaya kwa watoto wanaotamani kuwa wachezaji hapo baadaye.

Watoto wanaowaangalia wachezaji wakubwa wa sasa kama Aucho, hutamani kujifunza vitu vingi ili nao waje kuwa wachezaji wakubwa. Wanapoona matukio kama hayo halafu wanaoyafanya wanapewa tuzo, picha wanayopata ni kuwa matukio hayo siyo kitu kibaya…hii siyo ari ya mchezo (spirit of the game).

Tunajua kwamba dunia nzima tuzo zimekuwa changamoto, wasiostahili kuwemo kwenye orodha hadi kushinda na wanaostahili kutokuwemo. Kwa mfano kwenye fainali ya Kombe la Shirikisho la CRDB kule Zanzibar, kipa wa Azam FC, Mohamed Mustafa, alistahili kushinda tuzo ya mchezaji bora wa mchezo lakini hakupewa.

Hata tuzo hizi za sasa anazolalamikia Aucho, pia zina hilo tatizo, kwa mfano, kuachwa kwa Pascal Msindo siyo kitu sahihi.

Msindo amecheza vizuri sana msimu uliopita na alistahili kuwemo kwenye tuzo hizi au angalau kutolewa maelezo kukosekana kwake, lakini siyo Aucho. Pia Kipre Jr. wa Azam FC ametajwa kuwania tuzo ya kiungo bora, lakini kiufundi Kipre Jr. hakucheza mechi nyingi kama kiungo msimu uliopita.

Katika mechi 30 za msimu mzima, Kipre Jr. alicheza chini ya mechi 10 kama kiungo. Kwa asilimia kubwa alicheza kama mshambuliaji wa kati, hasa mzunguko wote wa pili.

Na bahati mbaya kwake mzunguko wa kwanza hakupata nafasi ya kucheza katika mechi nyingi, aidha alitokea benchi au hakucheza kabisa.

Kwa hiyo Kipre Jr. alistahili zaidi kuwania tuzo ya mchezaji bora wa jumla kwa sababu alifanya vizuri sana, lakini siyo kiungo bora. Na hao ni wachache na hayo ni mambo ya kiufundi, lakini kwa Khalid Aucho, hapana…hakustahili hata chembe.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live