Mabingwa watetezi wa Kombe la Mataifa ya Amerika Kusini, Argentina imekuwa ya kwanza kutinga robo fainali ya michuano hiyo inayofanyika Marekani baada ya kushinda mchezo wake wa pili dhidi ya Chile kwa bao 1-0.
Argentina inaongoza kundi A ikiwa na pointi 6 baada ya michezo miwili, ikifuatiwa na Canada yenye pointi 3, Chile pointi 1 na ya mwisho kundi hilo ni Peru yenye pointi 1.
Bao la Argentina limefungwa na Lautaro Martinez katika dakika 88 ya mchezo baada ya nahodha Lionel Messi kuchonga kona iliyosababisha piga nikupige langoni mwa Chile kisha Martinez kupata nafasi ya kutikisha wavu kwenye uwanja wa MetLife uliopo Jimbo la New Jersey uliokuwa na mashabiki 81,106.
Mchezo wa mwisho wa Argentina wa makundi utakuwa Juni 29 dhidi ya Peru kwenye uwanja wa Hard Rock uliopo jiji la Miami, Jimbo la Florida.