Timu ya Taifa ya Argentina imefanikiwa kutinga hatua ya Robo Fainali ya Michuano ya Kombe la Dunia inayoendelea nchini Qatar.
Argentina wanatinga hatua hiyo baada ya Jana Disemba 3, kufanikiwa kuondoka na ushindi wa mabao 2-1 mbele ya Australia katika dimba la Ahmed bin Ali nchini Qatar.
Mabao ya Argentina katika mchezo wa jana yamefungwa na Nahodha Lionel Messi dakika ya 35 na Julian Alvarez dakika ya 57 kipindi cha pili baada ya makosa ya Mlinda lango wa Australia Mathew Ryan kushindwa kuudhibiti mpira na kumkuta mfungaji.
Bao pekee la Australia limefungwa na Enzo Fernandes likiwa ni la kujifunga baada ya kugusa mpira uliokuwa umepigwa na mchezaji wa Australia na kumpoteza uelekeo mlinda mlango wake Emiliano Martinez.
Bao alilofunga Lionel Messi jana ndio bao lake la kwanza hatua ya mtoano katika michuano ya Kombe la Dunia ambayo ameshiriki mara tano kuanzia mwaka 2006, 2010, 2014, 2018 na 2022.
Hili ni goli la tisa kwa messi katika michezo 22 huku mpaka sasa akiwa amefunga mabao 789 katika michezo 1000 aliyocheza katika soka.