Nyota wa timu ya taifa Ujerumani na klabu ya Real Madrid, Antonio Rudiger anahusishwa na shirika la kigaidi kutokana na picha yake ambayo amevalia vazi jeupe kwenye mkeka huku akiwa anafanya maombi.
Muislamu huyo mcha Mungu, alionekana akifanya maombi na kisha aliandika ujumbe kwa Waisilamu. 'Mola Mtukufu atukubalie swaumu na sala zetu.' Huku akiwa amenyoosha kidole cha Shahada juu.
Picha hiyo imeonekana kutafsiriwa vibaya na baadhi ya watu, huku wakidai anajihusisha na mashirika ya kigaidi. Wapo wanaoamini kuwa kidole cha shahada kilichoinuliwa ndicho ambacho magaidi duniani kote wanakitumia kusherehekea mauaji yao.
Kutokana na hali hiyo, mchezaji huyo pamoja na Chama cha Soka cha Ujerumani wapo tayari kuchukua hatua za kisheria.