Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Alonso, mwite profesa wa boli

Xabi Alonso .jpeg Alonso, mwite profesa wa boli

Wed, 21 Feb 2024 Chanzo: Mwanaspoti

Mwite ‘Profesa wa Boli’. Huyo ni Xabi Alonso. Wakati anacheza kiungo katika klabu za Liverpool na baadaye Real Madrid na timu ya taifa ya Hispania, alikuwa anatisha ile mbaya. Na sasa akiwa kocha shughuli yake mmeisikia huko Ujerumani.

Lakini licha ya kufanya makubwa ya kihistoria, kocha huyo wa Bayer Leverkusen, amekataa kusherehekea baada ya timu yake kuifikia rekodi ya kucheza mechi nyingi zaidi bila ya kupoteza kwa timu ya Bundesliga kufuatia ushindi wa 2-1 ugenini dhidi ya Heidenheim wikiendi iliyopita.

Leverkusen ilipata ushindi wa 18 katika mechi 22 za ligi na kuweka pengo la pointi nane kati yake na mabingwa Bayern Munich walio katika nafasi ya pili, hivyo kufikisha mechi 32 bila ya kupoteza katika michuano yote msimu huu.

Hivyo wameifikia rekodi ya muda wote iliyowekwa na kikosi cha Bayern cha kocha Hansi Flick kati ya msimu wa 2019-20 na 2020-21.

“Sitasherehekea siku 500 za mafanikio haya,” alisema Alonso, ambaye alichukua mikoba kuifundisha Leverkusen Oktoba 2022 wakati klabu hiyo ikiwa katika ukanda wa kushuka daraja.

“Nimefurahishwa na mechi tuliyocheza, kwa kiwango tulichoonyesha na matokeo tuliyopata.

“Tuko katika wakati mzuri. Tutaendelea kupambana na kuweka akili kwenye mechi moja baada ya nyingine.”

“Kiujumla kiwango kilikuwa kizuri. Nina furaha, lakini tunapaswa kusonga mbele.”

Hakuna timu ambayo imewahi kumaliza msimu mzima wa Ligi Kuu ya Ujerumani bila ya kupoteza mchezo.

Kuna mechi 12 zimebaki kumaliza msimu huu. Tangu Alonso apewe Leverkusen, timu yake imevuna pointi 100 kutoka katika mechi 47 za Bundesliga, wastani wa pointi kwa mechi ambao unapitwa na Bayern iliyofudishwa na Pep Guardiola, Carlo Ancelotti na Flick tu.

Kiungo Granit Xhaka amesema “takwimu hazidanganyi” baada ya ushindi wao huo dhidi ya Heidenheim ambao umeendelea kuwaweka katika nafasi ya kuandika historia.

“Timu iko katika ubora wa juu. Tumeonyesha ni namna gani tunaweza kutawala,” alisema kiungo huyo wa zamani wa Arsenal.

Leverkusen, ambayo iliichakaza Bayern 3-0 wiki moja iliyopita, haijawahi kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Ujerumani licha ya kumaliza katika nafasi ya pili mara tano.

Leverkusen ya Alonso imeangusha pointi nane tu kati ya 66 ilizowania msimu huu. Pointi 58 ilizonazo zinaiweka katika nafasi ya tatu kwa ubora kufikia hatua hii ya msimu katika historia ya Bundesliga, nyuma ya Bayern ya Guardiola ya 2013-14, ambayo ilikusanya pointi 62, na pia ile Bayern yake Pep ya msimu wa 2015-16, ambayo ilikusanya pointi 59.

Chanzo: Mwanaspoti