Ally Kamwe, Ofisa Habari wa Yanga SC, amesema watawachagulia dozi ya kuwapa watani zao wa jadi Simba SC kutokana na namna watakavyokuwa.
Leo Jumapili, Yanga inawakaribisha Simba katika mchezo wa Ligi Kuu Bara unaotarajiwa kuchezwa Uwanja wa Mkapa, Dar.
Kamwe amesema ushindi wa Simba dhidi ya Yanga ni sare, hivyo wao watakachofanya ni kuwachagulia dozi kutokana na namna wapinzani wao watakavyokuwa.
“Tumeweka rekodi ya kutofungwa kwenye mechi 42 za ligi mfululizo, mchezo wetu dhidi ya Simba utakuwa wa 43 bila kufungwa, tumejipanga na tumejiandaa kupata ushindi. Hilo lipo wazi.
“Tutawachagulia dozi kutokana na namna watakavyokuwa kwani hata mgonjwa anapewa dozi kutokana na kile ambacho anaumwa, usiku wa Jumapili kuanzia saa mbili itakuwa ni muda wa furaha kwa mashabiki wetu,” alisema Kamwe.