STRAIKA wa KMC, Salim Aiyee amesema licha ya msimu huu kuumaliza vibaya ila umemuachia funzo la kujipanga vyema kuhakikisha ligi ijayo anakuja kwa kasi ya kufunga mabao mengi.
Aiyee amesema mejeraha yalimfanya akae kwa muda mrefu nje ya dimba, hivyo alijikuta hata akipewa nafasi ya kucheza anashindwa kucheka na nyavu kama misimu mingine iliyopita.
KMC ilimsajili Aiyee akitokea Mwadui FC, ambako kabla ya kusajiliwa KMC alikuwa amefunga mabao 19, akiwa nyuma ya Meddie Kagere aliyekuwa kinara wa mabao 23 na msimu huu pia amemaliza na 22.
"Nafasi ninayocheza ni ya kufunga, hata ningecheza kiasi gani bila kufunga ngumu kueleweka kwamba nilikuwa nafanya nini msimu huu,hilo nalichukua kama changamoto ya kuongeza bidii,"
Ameongeza kuwa "Nina tabia ya kujitathimini ambacho nimekifanya kwa msimu mzima, hilo linanisaidia kujituma na kujua nini niongeze na nini niachane nacho,"amesema.
Msimu huu amemaliza na bao moja, alilofunga dhidi ya Yanga, amesema anaamini hilo halitajirudia kwa kuwa yupo fiti, hivyo anaamini atafanya maandalizi kama inavyotakiwa.