Mwanachama wa Simba SC, Agnes Daniel ‘Aggy Simba’ amesema kitendo cha timu hiyo kupoteza ubingwa mara tatu, imekuwa sababu ya msimu huu kufanya usajili wa nguvu.
Akizungumza nasi, Agnes amesema Simba SC inataka kutengeneza kikosi kitakachokuwa tishio Afrika.
“Usajili ni kama kamari unaweza kupatia au ukakosea nafikiri ni muda wa kuwaunga mkono walioingia na bench la ufundi kwenda kutengeneza kilicho bora,” amesema Aggy Simba.
Licha ya maboresho ya kikosi Aggy Simba amewaomba wanachama na mashabiki kushusha matarajio.
“Kikubwa tuwaombee wachezaji wetu ‘pre season’ iwe bora kwao tujenge kikosi bora kuanzia ‘physic yao, ‘chemistry’ tupate muunganiko bora, ‘tactics’ za mwalimu ziwaingie mapema.
Pia amempongeza Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa klabu hiyo Mohammed Dewji kwa kurejea kwenye nafasi yake hiyo.
“Usajili mkubwa ambao wanasimba tunaufurahia sasa asikate tamaa na timu yetu na tunajua yeye ni simba damu na ataendelea kuipambania Simba turudishe heshima yetu ilopotea ya kukosa ubingwa kwa miaka mitatu,” ameongeza.