Dar es Salaam. Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam limewatahadharisha viongozi na waumini kuwa makini na watu wanaotumia jina la Askofu wa Jimbo hilo, Yuda Thadei Ruwa’ichi kutapeli.
Taarifa iliyotolewa jana Alhamisi Septemba 26, 2019 na katibu mkuu wa Jimbo hilo, Padri Frank Mutavangu imesema kuna watu wamefungua akaunti ya mtandao wa kijamii wa Facebook kwa jina la Askofu Mkuu Ruwa’ichi na kuomba michango kwa ajili ya ujenzi wa makazi ya malezi ya wajane, yatima na wakongwe.
“Napenda kuwatahadharisha kuwa kuna matapeli wamefungua akaunti ya Facebook kwa jina la Askofu, akaunti hii ni ya kitapeli."
“Baba Askofu Mkuu hajawahi kuomba mchango wa namna hii kwa njia hii na akaunti hii sio yake, naomba tujitahadhari na utapeli," inaeleza taarifa hiyo.
Padri Mutavangu amesema tayari wameripoti kituo cha polisi na kuwaomba wananchi kuwasiliana na ofisi ya Jimbo watakapokuwa na wasiwasi wakiona matangazo au maombi yanayohusu fedha.