Arusha. Watanzania wametakiwa kuitumia sikukuu ya Krismasi na mwaka mpya kuhimiza amani kuanzia ngazi ya familia zao hadi Taifa ili kuenzi kuzaliwa kwa Yesu Kristo.
Akitoa mahuburi leo katika ibada ya Krismasi katika Kanisa la Arusha International Baptist, Mchungaji kiongozi wa kanisa hilo, Profesa Harison Olang amesema ujumbe wa amani ndiyo mkubwa katika maadhimisho ya Krismasi.
Amesema ili kuleta utulivu na maendeleo katika taifa lolote kunapaswa kuwepo amani kuanzia ngazi ya familia, mitaani na Taifa.
Mchungaji Kiongozi Olang amesema hivi sasa kuna tatizo katika jamii, watu wanaabudu mali kuliko Mungu jambo ambalo halina faida katika maisha ya baadaye.
"Tusiabudu mali kuliko Mungu, kwa moyo na dhat, wanaobarikiwa ni wale wanaotangaza habari njema ya amani, tukumbuke ujumbe wa kwanza baada ya Yesu kuzaliwa ilikuwa ni amani," amesema
Amesema matatizo yanayoendelea katika mataifa mengi duniani kwa sasa hayawezi kumalizwa bila kujitokeza watu hadharani na kuhubiri amani ya kweli na kuwafikia watu wote.
"Kuna kiza dunia maafa yanaendelea kutokea hivyo kulingana na mazingira ya Krismasi ilikuwa usiku wa giza na watu walipelekewa ujumbe wa habari njema ya kuzaliwa Yesu Kristo kama mkombozi," amesema
Amesema kuzaliwa kwa Yesu kuendelee kuleta mwanga wakati wa giza ulimwengu mzima na wanaobarikiwa ni wale wanaolitii neno la Mungu.