Dini

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Wanasiasa waonywa kuwa chanzo cha vurugu

Edcbeb61f8b83463ebd52c4a175ddaba.jpeg Wanasiasa waonywa kuwa chanzo cha vurugu

Thu, 22 Oct 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

VIONGOZI wa Kamati ya Amani inayoundwa na viongozi wa dini mkoani Shinyanga, wamewataka wanasiasa kuacha kutumia lugha za kibaguzi, jambo ambalo linaweza kuleta uvunjifu wa amani.

Kaimu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Shehe Khalfan Ally aliyasema hayo jana alipozungumza na waandishi wa habari, akisema wanasiasa wasiwe chanzo cha kuchochea na viongozi wa dini wasioneshe mahaba yao kwenye nyumba za ibada.

Shehe Ally aliwataka wanasiasa na viongozi wa dini kuacha kutumia lugha za kibaguzi na viongozi wanapoendesha ibada wasivae mavazi yanayoashiria vyama fulani kwani wao ndio wanaoongoza nyoyo za watu wote, wakiwemo wenye imani na vyama tofauti ili kupoza machungu yao kwa kueneza amani.

“Kwani tunapokwenda kwenye nyumba za ibada tunakuwa pamoja hakuna ubaguzi wa aina yoyote, hivyo viongozi wa dini na wanasiasa kitu ambacho sio cha uadilifu ni kwenda kwenye nyumba za ibada na kuonesha mahaba ya chama fulani,” alisema kiongozi huyo wa kidini.

Aliwataka wananchi wajitokeze kwenda kupiga kura huku akiitaka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ifanye kazi yao kwa uadilifu isitokee mizozo ya aina yoyote na atakayechaguliwa ujue kwamba kawekwa na Mwenyezi Mungu.

Mchungaji John Kalinda wa Kanisa la Wasabato ambaye ni Mjumbe wa kamati hiyo, alisema wananchi wamekuwa na mshikamano mkubwa kwa kutembeleana kwenye misikiti na makanisa na mfumo wa vyama vingi umewekwa kikatiba kwa lengo la kuchochea maendeleo na waumini wana itikadi zao tofauti hivyo wanasiasa wasiwe chanzo cha kuvuruga amani.

“Tumekuwa tukifanya kazi bila kuwagawa waumini na tumekuwa wamoja, wanasiasa wasivuruge amani kwa maneno yao, bali waeleze sera na wasijaribu kuleta machafuko kwani nimetembea nchi nyingi Afrika hakuna amani. Amani imebaki nchi ya Tanzania tu,” alisema Mchungaji Kalinda.

Mjumbe mwingine ambaye ni Shehe wa Wilaya, Soud Kategile alisema dini inataka amani, inataka wananchi wajitokeze wapige kura kwa amani kwani ikivunjika haina mbadala na itakapotokea ni kuteseka watu wote.

Mchungaji Davidi Yegela ambaye pia ni mjumbe, aliwataka wanasiasa kunadi sera zao si matusi na kuendelea kulinda amani. “Kama kiongozi wa dini ningependa wananchi wajitokeze kupiga kura kwa amani nakurudi nyumbani kusubiri matoko,” alisema.

Chanzo: habarileo.co.tz