Dini

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Wakristo wazingatie mafundisho Pasaka

4fb4cf5f2142e87ef5392ce0ab83a0f9.jpeg Wakristo wazingatie mafundisho Pasaka

Mon, 5 Apr 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

LEO Wakristo wanamalizia sherehe za Sikukuu ya Pasaka mwaka huu.

Hii ni sikukuu ya kumbukumbu ya mateso, kifo na ufufuko wa Yesu Kristo yapata miaka milioni mbili iliyopita.

Kwa kawaida, sikukuu hii huja baada ya mfungo wa Kwaresima unaodumu kwa siku 40.

Katika Kipindi cha Kwaresma, Wakristo hujinyima mambo mbalimbali kadiri kila mmoja anavyoona inafaa huku wakijutia dhambi walizofanya na kumuomba Mungu awasaidie wasirudie.

Hiki ni kipindi ambacho Wakristo hujinyenyekeza zaidi mbele za Muumba wao na kuomba kuendeleza unyenyekevu huo huku wakiwa na maombi mbalimbali kwa ajili ya haja zao.

Kimsingi, katika kipindi chote hicho cha Pasaka, Wakristo wamekuwa wakishiriki ibada mbalimbali na kupata mafundisho mbalimbali ya kuwajenga kiroho.

Pasaka mwaka huu imeadhimishwa huku taifa likiwa katika maombolezo ya siku 21 kutokana na kifo cha Rais wa Awamu ya Tano, John Magufuli aliyefariki Machi 17, mwaka huu.

Katika sherehe za Pasaka kama ilivyo ada, yamekuwa yakitolewa mafundisho mbalimbali ya kiroho ili kuwaimarisha waumini kiimani na kujenga upendo miongoni mwa jamii.

Ndiyo maana ninasema, Mfungo wa Kwaresma na maadhimisho ya Sikukuu ya Pasaka mwaka huu yafungue ukurasa mpya wa maisha ya kila mmoja kujitafakari namna anavyoishi katika ulimwengu huu kwa nafasi yake.

Wakristo na wote wenye mapenzi mema, wazingatie mafundisho mbalimbali yaliyotolewa katika kipindi hiki ili Sikukuu ya Pasaka ili yawe na tija kiroho na hivyo kuiimarisha jamii.

Kuyazingatia ni hasa kuyaishi na kuyaendeleza mema yote waliyoyafanya waamini wakati wa mfungo wa Kwaresima na kuyaishi mafundishio yalitolewa na viongozi wa dini sambamba na kuwatii viongozi kwani viongozi hutoka kwa Mungu hasa walioingia madarakani kwa mujibu wa taratibu zilizopo kama katiba na uchaguzi.

Viongozi mbalimbali wamesisitiza pongezi zao kutokana na utulivu na ukomavu wa nchi katika kipindi cha maombolezo hali inayoonesha wanaisikia sauti ya Mungu juu yao na hivyo, waendelee kuisikia na kuitii ili kudumisha imani zao na amani katika jamii.

Wakristo wafuate mfano wa Yesu kwa kuwa watu wa msamaha, wasiolalamika na pia wasiwe watu wa ‘maneno mengi’ wanapopita katika hali ngumu.

Kiimani, kumaliza mfungo wa Kwaresima na sherehe za Pasaka si kwamba ndio mwisho wa kuisikia sauti ya Mungu na kuishi kwa upendo na unyenyekevu kwa Mungu, bali hasa ndo mwanzo wa unyenyekevu, upendo, huruma, matoleo na kuomba zaidi huruma ya Mungu huku kila mmoja akijitahidi asiangukie dhambini alikokuwa.

Ndiyo maana ninasema, kila mmoja kwa nafasi yake ayabebe na kuyafanyia kazi mafundisho ya dini yakiwamo hasa yaliyotolewa katika kipindi cha Pasaka, huku akitambua kuwa ukiukaji wowote wa Amri 10 za Mungu, kukosa uadilifu na kuendekeza kiburi na hata ubadhilifu, ni kutaka kumuua Yesu Kristo tunayesherehekea ufufuko wake.

Chanzo: www.habarileo.co.tz