KATIKA kuuaga mwaka 2020 na kuukaribisha mwaka mpya 2021, viongozi wa madhehebu ya Kikristo wamendaa dua maalumu kwa taifa, itakayofanyika leo usiku Dar es Salaam wakati wa mkesha wa kitaifa wa mwaka mpya.
Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Kamati inayoratibu mkesha huo na mingine inayofanyika katika mikoa saba ya Tanzania Bara na Tanzania Visiwani, Askofu Godfrey Emmanuel, katika mkoa wa Dar es Salaam dua hiyo itafanyika Uwanja wa Uhuru.
Alisema pamoja na kuuombea mwaka mpya, dua hiyo itafanyika kumshukuru Mungu kwa upendo wake wa kuliwezesha taifa kuushinda ugonjwa wa Covid 19, unaosababishwa na virusi vya corona.
“Huu ni mkesha mkubwa wa kitaifa ambao huwa maalumu kwa ajili ya Watanzania wa imani zote kufanya maombi maalumu kuliombea taifa kupita katika mikono salama kwa kipindi chote” alisema Askofu Emmanuel.
Alisema tangu kuanza kwa utaratibu wa maombi hayo mwaka 1997, kumekuwa na mafanikio makubwa ikiwemo kuwaunganisha Watanzania kwa kuhubiriana kuhusu amani na upendo.
“Dua hiyo zaidi imelenga kuliweka taifa mikononi mwa Mungu, tunamshukuru Mungu kwa kuwa kila mwaka washiriki wamekuwa wakiongezeka, jambo linaloashiria kukubalika vyema kwa uwepo wa maombi hayo”alisema.
Alisema mbali na Dar es Salaam, dua hiyo itakayoambatana na mkesha huo itafanyika mikoa ya Kilimanjaro, Arusha, Dodoma, Iringa, Singida na Zanzibar. Alitoa mwito kwa Watanzania wa imani zote, kujitokeza kwa wingi kushiriki katika dua hiyo.
Askofu Emmanuel aliwapongeza Watanzania kwa kuendelea kudumisha amani na utulivu wakati wote, kwa kuwa hiyo ndiyo njia pekee ya taifa kupiga hatua muhimu ya maendeleo.