Dar es Salaam. Viongozi mbalimbali nchini Tanzania wameshiriki ibada ya mazishi ya mkurugenzi mstaafu wa Idara ya Usalama wa Taifa (Tiss), Apson Mwang’onda katika Kanisa Katoliki la St Peters, jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi huyo wa zamani wa Tiss alifariki dunia Jumatatu Oktoba 7, 2019 nchini Afrika Kusini alikokuwa akitibiwa na mwili wake umesafirishwa leo kwenda wilayani Mbozi mkoani Mbeya kwa maziko.
Viongozi waliohudhuria ibada hiyo ni marais wastaafu, Jakaya Kikwete na Ali Hassan Mwinyi; Katibu Mkuu Kiongozi, John Kijazi, Waziri Mkuu mstaafu, Cleopa Msuya na Katibu Mkuu mstaafu wa CCM, Abdulrahman Kinana.
Wengine ni Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama (CDF), Jenerali Venance Mabeyo; CDF mstaafu George Waitara; ma Inspekta Jenerali wastaafu wa polisi, Omary Mahita na Said Mwema, mkurugenzi mkuu wa Tiss, Diwani Athuman pamoja na mtangulizi wake Dk Modestus Kipilimba.
Wengine ni mwenyekiti mstaafu wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), Damian Lubuva na Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Daniel Chongolo, wabunge Anna Tibaijuka (Muleba Kusini), Peter Serukamba (Kigoma Kaskazini), William Ngeleja (Sengerema), Mwigulu Nchemba (Iramba), James Mbatia (Vunjo) na mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mghwira.
Msemaji wa familia, Amos Mataluma amesema Mwang'onda alianza kufanya kazi Tiss mwaka 1973 akitumikia nafasi mbalimbali kabla ya kuteuliwa na Rais mstaafu Benjamin Mkapa mwaka 1996 kuwa mkurugenzi mkuu wa idara hiyo.
Pia Soma
- Alat yaonya matangazo uchaguzi Serikali za mitaa
- Vipengele vitatu vyaongezwa tuzo za Ejat
- Kikwete afafanua alichomaanisha kwenye hotuba yake