Mwanza. Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo la Mwanza, Renatus Nkwande amesema viongozi wa dini na Serikali wana wajibu wa kupinga na kukemea mambo yanayoendelea nchini kutoka nchi za Magharibi kama ushoga na utoaji mimba.
Askofu Nkwande ametoa kauli hiyo leo Jumapili Mei 12 baada ya kusimikwa kuwa askofu mkuu wa jimbo hilo.
"Tuwasaidie wananchi wapate elimu na kuwaondolea hofu, tuwakomboe katika kweli na kiroho kila mtu awe mwalimu, kwa sasa Afrika tumeanza kuiga mambo ambayo hata hayafai ikiwamo ushoga na kutoa mimba.”
"Leo kuna taasisi zinazunguka na kuhamasisha kutoa mimba lakini hakuna anayezungumza hata Serikali mkibanwa kidogo mnalegeza, tupiganie uhuru kwa kukataa ushoga na kutoa mimba,” amesema.
“Japokuwa najua watu hao ni wakali lakini sitaogopa wala kupata hofu kuzungumzia mambo hayo na kuyakemea tushikane wote,” amesema.
Akisisitiza kuwapo kwa ushirikiano kati ya Serikali na taasisi za dini amesema: “Yapo mambo mengi yanayofanywa na kanisa Katoliki mfano ni Hospitali ya Rufaa ya Bugando na Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino (Saut), hivyo tunahitaji ushirikiano wa Serikali katika kuendeleza huduma hizo kuanzia ngazi ya jamii.”