BARAZA Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata) limetangaza kuwa sikukuu ya Idd El Fitr itakuwa Alhamisi Mei 13 au Ijumaa Mei 14, mwaka huu, kutegemea kuandama kwa mwezi.
Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa baraza hilo Nuhu Mruma, sherehe za Idd El Fitr kitaifa kwa mwaka huu zitafanyika mkoani Dar es Salaam na swala ya Idd itaswaliwa katika viwanja vya Mnazi Mmoja kuanzia saa 1:30 asubuhi.
Alisema pia Baraza la Idd litafanyika katika viwanja vya Karimjee kuanzia saa 8:00 mchana na mgeni rasmi anategemewa kuwa Rais Samia Suluhu Hassan.
“Kwa niaba ya Bakwata Mufti na Shehe Mkuu wa Tanzania Abubakari Zubeir (pichani) anawatakiwa waislamu na watanzania wote sikukuu njema na anawaomba wote kusherehekea kwa usalama na amani,” alisema Mruma.
Sikukuu ya Idd ni moja ya sherehe muhimu kwenye kalenda ya Uislamu huashiria kumalizika kwa mwezi Mtukufu wa Ramdhan na huadhimishwa kwa ibada ya swala, dhifa za chakula na manunuzi ya zawadi pamoja na mavazi.
Mwaka jana sikukuu hiyo, iliadhimishwa Juni 5, mwaka huu ambako kitaifa iliswaliwa mkoani Tanga na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alikuwa mgeni rasmi.