Dar es Salaam. Rais wa Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC), Askofu Gervas Nyaisonga amewetaka Watanzania na Wakatoliki kutoshtuka na vifo vya maaskofu wastaafu Gabriel Mmole na Emmanuel Mapunda kwa sababu ni vifo vyema.
Askofu mstaafu, Gabriel Mmole aliyekuwa Jimbo la Mtwara alifariki dunia Mei 15, 2019 akiwa anaumwa huku Askofu Emmanuel Mapunda aliyekuwa jimbo katoliki la Mbinga akifariki dunia jana.
Nyaisonga ambaye pia ni askofu wa Jimbo Kuu la Mbeya ametoa kauli hiyo leo, Mei 17, 2019 wakati akizungumza na Mwananchi.
Askofu Nyaisonga amesema: “Watu wasishtuke sana, hawa waliofariki ni maaskofu wetu waliotumikia na wana umri wa zaidi ya miaka 80. Sasa unajua unapokuwa mzee mwili unakuwa dhaifu kiasi, wasishtuke ni vifo vyema na vimewakuta katika uzee na ukiwa katika hatua hii mwili unaweza ukapata shida.
Amefafanua kuwa vifo vya maaskofu hao ni vya kusifiwa kwa sababu wametumikia kanisa na walipofikia miaka 75 walikabidhi vijiti, lakini waliendelea kuishi vizuri na wale maaskofu waliowarithi.
Hata hivyo, Askofu Nyaisonga ametumia nafasi hiyo kuwapa pole wanakatoliki akieleza kuwa hata mtu akiwa mzee bado anabaki kuwa mpendwa wao kwa sababu maaskofu hao walitegemewa kwa ushauri na hekima zao.
Pia Soma
- Taulo za kike hazina kodi Vat, bado bei ya juu
- Mchungaji Msigwa ahoji uhalali Ndugai kumsimamisha mbunge CCM
Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Tec, Padri Charles Kitime mazishi ya Askofu Mmole (80) yatafanyika Mei 21, mwaka huu Mtwara, wakati Mapunda (84) atazikwa Mei 24 wilayani Mbinga.