Dar es Salaam. Mchungaji wa Kanisa la EAGT la Mtamba wilayani Kisarawe mkoani Pwani, Shauri Steven anashikiliwa na polisi kwa tuhuma za kumbaka na kumpa mimba mwanafunzi wa darasa la tano.
Mwanafunzi huyo amebakwa na kupewa mimba wakati takwimu zikionyesha mwanafunzi mmoja kati ya watatu amekatisha masomo kwa mimba au ndoa za utotoni.
Akizungumza na Mwananchi jana Jumanne Desemba 17, 2019 Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe, Jokate Mwegelo amesema sababu za mchungaji huyo kubaka na kumpa mwanafunzi mimba ni tamaa za mwili.
Alisema mchungaji huyo alifanikiwa kumlaghai mwanafunzi kwa madai ya kumfanyia huduma ya maombi.
Jokate ambaye ni Mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama wa Wilaya ya Kisarawe alisema Desemba 12, 2019 mwalimu wa shule ya msingi Mtamba, Justine Mrutu aligundua mwanafunzi huyo mjamzito.
"Alimlaghai kupitia mbinu ya maombi, mtuhumiwa amekamatwa na atafikishwa mahakamani," alisema Jokate.