PAROKIA ya Mtakatifu Rita wa Kashia ya Mbezi Temboni, Dar es Salaam imemuaga Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads), Patrick Mfugale , aliyefariki dunia Jumanne akitajwa kuwa alikuwa muumini mwenye mchango mkubwa katika kanisa hilo.
Misa ya kumuaga iliongozwa na Paroko wa Parokia hiyo, Padre Joel Nziku aliyemwelezea Mfugale kuwa alihudumu kwa moyo mkunjufu huku akijituma kwa hali na mali.
“Mfugale ni kati ya waumini ambao wamekuwa na mchango mkubwa katika uanzishwaji wa Parokia hii, amekuwa akijituma na kufanya kazi za kanisa kwa moyo mmoja. Hakika Parokia inamlilia kwa uwezo wake mkubwa katika kuongoza waumini na kutenda kazi yake Mungu,” alisema Padre Nziku.
Alisema tangu mwaka 2005 kikiwa Kigango, Mfugale alikuwa kati ya waumini wachache waliochangia kuanzishwa kwa Parokia .
Miongoni mwa viongozi wa serikali waliohudhuria misa hiyo ni pamoja na Waziri wa Katiba na Sheria, Profesa Palamagamba Kabudi na Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Dk Leornard Chamuriho.
Mwili wa Mfugale ulisafirishwa jana kwenda Ifunda mkoani Iringa kwa ajili ya maziko yatakayofanyika kesho kwenye makaburi ya familia.
Leo wanafamilia na wakazi wa mkoani Iringa watakuwa na wasaha wa kumuaga na kufanya ibada .