Dar es Salaam. Katika kukabiliana na kasi ya maambukizi ya ugonjwa wa virusi vya corona (CODIV-19), Baraza la Ulamaa nchini Tanzania limetoa maelekezo 11 kwa Waislam wote.
Pamoja na maelekezo hayo, baraza hilo litachukua hatua zaidi endapo kasi ya maambukizi itaongezeka nchini humo na kuhatarisha maisha ya Watanzania.
Maelekezo hayo ni pamoja na kufunga madrasa zote kufutia agizo la Serikali la kusitisha masomo kwa shule na vyuo vyote hadi hapo itakapotangazwa.
Pia, baraza hilo limewataka Waislam kutii amri ya karantini pale itakapotolewa na mamlaka husika ili kuokoa nafsi zisiangamie.
Mufti wa Tanzania, Sheikh Abubakar Zubeir ametoa maelekezo hayo leo Jumatano Machi 18,2020 wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam akisema ni muhimu kuzingatia agizo la kuacha misongamano ili kuzuia ugonjwa huo usisambae.
“Kuokoa nafsi za wengine zisiangamie ni ibada kubwa na mtekelezaji wa amri na maagizo haya atalipwa thawabu zisizo kifani. Atakayepinga amri hizi akasababisha watu kuambukizwa na kufa ataandikiwa dhambi,” amesema
Habari zinazohusiana na hii
- VIDEO: Mgonjwa wa kwanza wa corona awaomba msamaha Watanzania
- Baadhi ya mabasi ya abiria yaanza kuchukua tahadhari ya corona
- Wagonjwa wa corona Tanzania wafikia watatu
- Watafiti Uganda wagundua virusi vya corona kwenye mwili wa ngamia na popo
Amesema kwa Mwislamu atayapatwa na maradhi hayo ni haramu kwake kuhudhuria swala za Ijumaa na swala za jamaa kama ambavyo ni haramu kwake kujichanganya na watu wengine.
Maelekezo mengine waumini wenye uwezo kwenda msikitini na miswala yao ili kupunguza uwezekano wa kuambukizana.
Mufti pia amewataka waumini wenye matatizo ya kiafya na wenye umri mkubwa ku swali majumbani kwa kuwa kundi hilo ndilo lipo kwenye hatari zaidi ya kuambukizwa.
Endelea kufuatilia Mwananchi kwa habari zaidi