Mtoto Saidi Ramadhani mwenye umri wa miaka 5 amefariki dunia papohapo na watoto wengine 3 kujeruhiwa vibaya sehemu mbalimbali za miili yao baada ya kuangukiwa na tenki lililopasuka ambalo limekuwa likitumika kuhifadhia maji ya kunawa kabla ya kuanza ibada katika Msikiti wa Salama mkoani Tabora.
Akizungumzia tukio hilo lilitokea jana jioni Imam wa msikiti huo, Shaban Mabula amesema ingawa tenki hilo lina nyufa hawakutarajia kuwa litapasuka na kuleta maafa hayo yaliyogharimu maisha ya mtoto huyo na kujeruhi wengine.
“Hapa palikuwa na watu wanne mkubwa mmoja na watoto watatu mtoto mmoja alipondwa na hilo tenki baada ya kupasuka akawa amepasuka kichwa na kuvunjika mguu wa kulia lakini pia hata uso wake ulikuwa umepasuka ikapelekea umauti wake “ amesema Imam Mabula
Akisimulia tukio hilo shuhuda mwingine amesema kabla ya kuanza kuswali msikitini hapo alisikia kitu kama bomu linalipuka na alipogeuka na kuchungulia dirishani akiwa ndani ya msikiti huo aliona maji yakiwa juu na alipotoka nje alikuta tenki hilo limepasuka na kuona watu wamekandamizwa na vipande vya matofali vya tenki hilo.