Unguja. Mkutano wa 15 wa baraza la tisa la wawakilishi Zanzibar unatarajiwa kuanza Jumatano Septemba 18, 2019 Chukwanje nje kidogo ya Mji wa Unguja.
Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari, leo Jumatatu Septemba 16, 2019, Katibu wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, Raya Issa Mselem amesema mkutano huo unatarajiwa kuanza kwa maswali na majibu.
Amesema jumla ya maswali 137 yanatarajiwa kuulizwa na wajumbe wa baraza la wawakilishi na kupatiwa majibu kutoka kwa mawaziri wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ).
“Mbali na maswali na majibu katika mkutano huo, shughuli nyingine itakuwa kusomwa kwa mara ya pili muswada wa sheria ya viongozi wa kitaifa na kutunga sheria ya kuanzisha jumuiya ya mawakili Zanzibar,”amesema.
Pia, amesema muswada mwingine ni wa Sheria ya Utawala wa Baraza la Wawakilishi.