Dini

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mgogoro KKKT wazidi kuvuruga majimbo

Mgogoro Edited Data Mgogoro KKKT wazidi kuvuruga majimbo

Mon, 28 Mar 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Hali bado si shwari ndani ya Dayosisi ya Konde ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) licha ya kumng’oa askofu wao, Edward Mwaikali huku wakuu wa majimbo, wachungaji na waumini wakigawanyika katika makundi mawili.

Wakati hali ikiwa hivyo katika dayosisi hiyo ambayo ni moja kati ya dayosisi 26 za KKKT, aliyewahi kuwa Askofu wa Dayosisi ya Kaskazini Mashariki, Dk Stephen Munga ametaja mambo manne ambayo anasema ndiyo yanalibomoa kanisa hilo nchini.

Askofu Mwaikali alivuliwa wadhifa huo katika mkutano mkuu maalumu ulioitishwa na Mkuu wa KKKT, Askofu Fredrick Shoo na kufanyika Machi 22, 2022, huku mikoba yake ikirithiwa na Geofrey Mwakihaba.

Hata hivyo, maamuzi hayo si tu kwamba yamepingwa na Askofu Mwaikali kuwa ni batili kwa mujibu wa Dayosisi ya Konde, lakini pia baadhi ya maaskofu wanaodai mkutano ulikuwa ni batili na mkuu wa Kanisa hakuwa na mamlaka kuuitisha.

Moto wa mgogoro huo unazidi kusambaa kwa wakuu wa majimbo, wachungaji na waumini huku wakigawanyika katika makundi mawili, moja likiafiki kilichotokea na kundi lingine likisimama na Askofu Mwaikali na halmashauri kuu yake.

Wakuu wa majimbo wagawanyika

Mkuu wa Jimbo la Mbeya Mashariki, Nyibuko Mwambola alieleza yeye na Askofu Dk Edward Mwaikali bado ni viongozi halali wa kanisa na hawatambui mkutano mkuu uliowaondoa.

“Mkutano huo ulikuwa wa kihuni. Hata mimi na mkuu wa Jimbo la Mbeya Magharibi, Mchungaji Judith Kajela tumeondolewa katika nafasi zetu kwa sababu ambazo hata Mkuu wa Kanisa Dk Shoo hawezi kuzitolea ufafanuzi,” alisema.

Mchungaji Mwambola alisema msimamo wao ni kutoachia nafasi hizo mpaka hapo kanuni, sheria na katiba ya Dayosisi ya Konde zitakapofuatwa, kwani wamepata taarifa za kwenda kuondolewa kinguvu na vyombo vya dola.

Hata hivyo, Mkuu wa Jimbo la Mwakaleli, Mchungaji Lugano Mwakasege alisema kuwa ukiukwaji wa katiba za kanisa ndio uliowafikisha hapo na mara kwa mara walimshauri Askofu Mwaikali wakae meza moja kumaliza tofauti lakini alikataa.

“Kuna wakati walifukuza zaidi ya wachungaji 25 wakashindwa kutoa huduma za kiroho kwa waumini. Sasa tunamshukuru Mkuu wa Kanisa kuingilia kati kulinusuru kanisa. Kama viongozi wa kanisa sasa tunashukuru kwa hatua hiyo,” alisema.

Mchungaji Mwakasege aliongeza kuwa mgogoro huo umewatia dosari wachungaji wa Dayosisi ya Konde na Serikali, na kwamba wanaomba ufike wakati tofauti zote ziwekwe pembeni na kukubali matokeo na kuacha kuchochea migogoro.

Kwa upande wake, Mkuu wa Jimbo la Kati Itete, mchungaji Kumbuka Mwasanguti aliomba ufike wakati viongozi wa pande zote mbili kumaliza mvutano na kuanza kushirikiana kuongoza waumini na kushirikiana na Askofu mteule Mwakihaba.

Mchungaji wa Dayosisi ya Tukuyu, Dk Stephen Kimondo yeye alisema wao ndio walikuwa waanzilishi wa mgogoro huo, baada ya kuandika barua kwa Mkuu wa Kanisa kuomba aingilie kati kufuatia mali za dayosisi kuhamishiwa Ruanda.

“Uchaguzi uliofanyika ni wa haki kwani awali uliletwa waraka kwa kutaka pande zote mbili kuteua wajumbe saba ili wakae kikao Machi 13 mwaka huu katika mji wa Makambako Mkoa wa Iringa, jambo ambalo lilipigwa chenga,”alisema.

Dk Kimondo ambaye kwa sasa ni mhadhiri wa Chuo Kikuu Iringa, alisema kutokana na kutofanyika kwa kikao hicho, ndipo halmashauri kuu ya kanisa ilipoitisha mkutano na kufanya uchaguzi wa haki na huru na kupata uongozi mpya.

Alisema maamuzi ya mkutano huo ni sahihi na yametokana na Askofu Mwaikali kuvunja katiba, hivyo ni wakati sasa wa kupumzika na kuepukana na kuchochea migogoro isiyokuwa na tija na kuwagawa waumini na kanisa kwa ujumla.

Askofu Munga ataja chanzo cha migogoro KKKT

Akizungumza na gazeti hili, Askofu Munga ambaye Dayosisi aliyokuwa akiiongoza nayo ilipitia katika mgogoro, alisema KKKT inabomolewa na majungu, visasi, hila na ulinzi wa maslahi binafsi na kuhoji kuwa iko wapi nguvu ya huduma na Utume.

“Je, iko wapi nguvu ya utume na ushuhuda wa Injili ya wokovu? KKKT imepoteza waumini wake wangapi kwa ajili ya migogoro na viongozi kutumika au kutumiwa vibaya,” alisema Askofu Munga ambaye bado ana mgogoro na uongozi mpya.

“Ni vema KKKT litafakari kwa maombi na kumsihi Bwana wa Kanisa awape maaskofu wake ujasiri wa kutengeneza mambo yaliyobomoka”, alisema. Kikao cha maaskofu wa KKKT kimepangwa kufanyika Jumatatu ya Machi 28.

Hoja za maaskofu wanaompinga Dk Shoo

Akizungumza na Mwananchi hivi karibuni, Askofu wa Dayosisi ya Ziwa Tanganyika ya KKKT, Ambele Mwaipopo, alisema mkutano huo mkuu maalumu ulioitishwa na mkuu wa Kanisa, haukuwa sahihi na kudai mkuu wa Kanisa amepoka mamlaka ya kikatiba ya Askofu Mwaikali.

“Kwa sababu nazifahamu katiba zote mbili ya Konde na ya KKKT ni kwamba kilichotokea Konde hakiko sawasawa kwa sababu kila dayosisi ina autonomy (ni huru na zina mamlaka kamili) ya kujiendesha zenyewe,” alisema Askofu Mwaipopo.

“Katiba zao zina namna ya kumuingiza askofu na kuna vyombo vya kikatiba ambavyo hata katiba ya KKKT inavitaja. Kila Dayosisi itakuwa na katiba yake, itakuwa na vyombo vyake vya maamuzi, halmashauri kuu na mkutano mkuu”

“Hivyo vyombo ndio vitaendesha shughuli, vita recruit (kuajiri) wachungaji, vitawapanga wachungaji, vitapanga kazi za umisioni kwa kutumia vyombo hivyo ambavyo ni halmashauri kuu na mkutano mkuu.

“Mkutano mkuu wa dayosisi unaandaliwa na Askofu wa Dayosisi akishirikiana na halmashauri kuu yake, kitu ambacho sasa pale Konde hakikufanyika hivyo ndio maana nasema kilichotokea pale Dayosisi ya Konde hakiko sawa,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Askofu wa Dayosi ya Karagwe, Dk Benson Bagonza alisema kwa muundo wa KKKT, askofu hajawahi kumfukuza au kumvua uaskofu askofu mwingine kwani huingia kwa mchakato na kuondoka kwa mchakato.

“Karibu mabaraza yote ya maaskofu wa kiprotestanti duniani hufuata kanuni ya the first among the equals (wa kwanza aliye sawa na wengine). Hata aliyewekwa wakfu jana ni sawa na aliowakuta,” alisisitiza Askofu Bagonza na kuongeza;-.

“Kwa utaratibu wa “kiundugu na kirafiki” heshima ya u-rika hufuatwa wakiwa wenyewe ndani lakini u-rika haumpi yeyote nafasi ya ziada juu ya wengine.

“Kilichotokea Konde ni kama hakikutokea. Historia ya kanisa haikunyooka, imejaa mabonde na milima, damu na kusalitiana. Hili litapita na kanisa litasimama. Kristo ndiye Mkuu wa Kanisa,” aliongeza kusema Askofu Bagonza alipozungumza na Mwananchi hivi karibuni.

Askofu Munga yeye mbali na kusema alichokifanya Askofu Shoo Konde hakikubaliki, lakini alihoji ni katiba gani inayotumika KKKT kwa sasa ambayo inaruhusu mkuu wa Kanisa kuingilia uendeshaji wa dayosisi nyingine.

Kwa upande wake, Dk Shoo tayari ameshasema kwamba suala hilo atalizungumzia rasmi hivi karibuni hili kuondoa utata huo.

Migogoro mingine iliyoitikisa KKKT

Mgogoro mwingine ambao uliwahi kuitikisa KKKT ni wa Meru mwaka 1990 hadi 1993 ambapo baadhi ya waumini walianzisha vuguvugu la kujitenga kutoka Dayosisi ya Kaskazini wakipinga mgawanyo usio sawa wa rasilimali na miradi.

Waumini hao walijenga hoja kuwa upande wa Uchagani ulikuwa unapendelewa na mgogoro huo ulisababisha vurumai nyingi hadi aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani wakati huo, Agustino Mrema kutumwa kuusuluhisha.

Mgogoro mwingine unaofanana na huo ni wa Dayosisi ya Pare, uliotokana na vuguvugu la waumini wa KKKT upande wa Wilaya ya Mwanga kufanya mchakato wa kuzaliwa kwa dayosisi mpya ya Mwanga, ambao baadaye ulizimwa na KKKT makao makuu.

Hali hiyo iliibua mvutano wa miaka 18 uliosababisha matukio ya uvunjifu wa amani, zikiwamo nyumba kuchomwa, hadi mwaka 2016 ambapo dayosisi hiyo ilizaliwa na kuhitimisha safari ya miaka 18 iliyoshuhudiwa wachungaji wakitengwa na kanisa.

Mgogoro mwingine ulioibuka ulikuwa ni Dayosisi ya Kaskazini Mashariki mwaka jana na kushuhudiwa Ofisi ya Mkuu wa Kanisa ikiunda kamati ya maaskofu wastaafu wanne, kusimamia uchaguzi wa askofu mpya wa dayosisi hiyo.

Hii inatokana na Askofu Dk Stephen Munga aliyekuwa akishikilia wadhifa huo kustaafu Machi, 2020 baada ya kutimiza umri wa miaka 65, lakini mkutano mkuu wa kutafuta mrithi wake ukachelewa.

Hata hivyo, licha ya uchaguzi wa askofu kufanyika, mgogoro uliendelea kwani Novemba mwaka huu halmashauri kuu ya dayosisi hiyo ilimsimamisha uchungaji Askofu Munga sambamba na wachungaji wengine saba waliokuwa enzi za Dk Munga.

Mwaka 2018 kuliibuka mgogoro mwingine uliolitikisa kanisa hilo baada ya kutokea mvutano wa kuzaliwa kwa dayosisi mpya ya Mufindi, lakini uongozi wa dayosisi ya Kusini uligomea uamuzi huo.

Kuanzia hapo, kulifuatiwa na matukio ya kutengwa kwa waumini wakidaiwa ni waasi na wengine kufunguliwa kesi polisi, vitendo ambavyo vilizidisha chuki na kuchochea zaidi mgogoro huo.

Mbali na huo, uliwahi kuibuka mgogoro ndani ya Dayosisi ya Ziwa Tanganyika, ulioanza 2017 kati ya washarika wa Mpanda na uongozi wa dayosisi, ambapo washarika walipinga kuhamishwa kwa mchungaji wao, Calvin Kessy.

Mgogoro huo ulifikia hatua mbaya Mei 2018, baada ya baadhi ya waumini kumzuia Askofu wao, Ambele Mwaipopo kuingia Usharika wa Sumbawanga mjini na inaelezwa tukio hilo liliambatana na msafara wake kurushiwa mawe.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live