Arusha. Hatimaye Bibi Nasi Muruo (98) mkazi wa eneo la Sinoni, jijini Arusha nchini Tanzania leo Jumanne Septemba 24, 2019 ameanza kupokea fidia ya ardhi yake kwa kulipwa kiasi cha Sh69.1 milioni kati ya Sh519.3 milioni anazopaswa kulipwa.
Fedha hizo zimetolewa na Kanisa la Evengalistic Assemblies of God Tanzania (EAGT) baada ya kuhangaikia kusaka haki yake kwa miaka 42.
Serikali ya Tanzania imezipa miezi mitatu kaya 110 zilizojenga kwenye ardhi ya kikongwe huyo kumlipa Sh519.3 milioni kutokana na ardhi ambayo inamilikiwa na kila kaya.
Akizungumza baada ya kukabidhiwa fedha hizo, Bibi Muruo alimshukuru Rais wa Tanzania, John Magufuli, Waziri wa Ardhi wa nchi hiyo, William Lukuvi kwa kumsaidia kupata haki yake.
“Naishukuru sana Serikali, leo nimeanza kupata haki yangu, baada ya kuitafuta kwa miaka 42, nitakula nyama leo,” amesema
Katibu Mkuu wa Kanisa la EAGT, Askofu Leonard Mwizarubi amesema kanisa hlo limeamua kumlipa kiasi chote cha fedha bibi huyo ili aweze kuishi maisha mazuri.
Pia Soma
- Moto wateketeza wodi ya wazazi, waua vichanga wanane
- Waziri Mkuu Uingereza apata pigo jingine
- Edda Sanga apewa tuzo ya heshima
Askofu Mwizarubi amesema kanisa limelipa fedha hizo kutekeleza maagizo ya Serikali kwa kuamini bibi huyo alikuwa na haki zote za umiliki wa eneo hilo ambalo alikuwa akigombania na ndugu yake.
“Kama kanisa tunampongeza Rais John Magufuli kwa uamuzi wa kumpa haki bibi huyu na sisi tunamuunga mkono,” amesema
Bibi huyo ambaye alikuwa anatetewa na Kituo cha Sheria na Haki za Binaadamu, Julai 2019, alitoa malalamiko katika gazeti la Mwananchi akimuomba Rais Magufuli kuingilia kati kumsaidia kupata haki yake kwani tangu ameshinda kesi ya kurejeshewa ardhi hiyo mwaka 1979 ameshindwa kupata haki yake.
Bibi huyo alipokonywa eneo lake na ndugu katika familia yao, Edward Lenjeshi ambaye hata hivyo mwaka 2017 alifariki duniani wakati bado shauri hilo lipo mahakamani.
SOMA ZAIDI
> Magufuli amrejeshea ardhi kikongwe baada ya kuidai kwa miaka 42
> Kikongwe aliyepigania ardhi yake kwa miaka 42 kulipwa milioni 500