Dini

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kardinali Rugambwa kukabidhiwa Kanisa Jimbo Kuu la Roma

KADINALI RUGAMBWA Kardinali Rugambwa kukabidhiwa Kanisa Jimbo Kuu la Roma

Sat, 17 Feb 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Kardinali Protase Rugambwa, “Kardinali Padre”, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Tabora, Dominika tarehe 18 Februari 2024, anakabidhiwa Kanisa la “Santa Maria in Montesanto”, lililoko kwenye Barabara la Babuino, namba 198, Roma, kuashiria kwamba, Kardinali Rugambwa sasa ni sehemu ya Wakleri wa Roma, wanaounda Baraza la Makardinali lenye jukumu la kumsaidia Khalifa wa Mtakatifu Petro katika shughuli zake za kichungaji kama Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Roma.

Makardinali kimsingi ndio washauri wakuu wa Khalifa wa Mtakatifu Petro ili kukoleza juhudi za toba, haki, amani na maridhiano; kwa kukuza na kudumisha utu na heshima ya binadamu, ili watu waweze kuishi katika mazingira bora zaidi.

Baba Mtakatifu Francisko Dominika tarehe 9 Julai 2023 aliwateuwa Makardinali wapya 21 kati yao Makardinali watatu ni wale ambao wamejipambanua katika huduma kwa Kanisa na watu wa Mungu katika ujumla wao.

Makardinali wapya wakasimikwa rasmi katika mkutano wa kawaida wa Makardinali ulioadhimishwa tarehe 30 Septemba 2023 mjini Vatican. Hawa ni Makardinali wanaoonesha ukatoliki wa Kanisa, wanaotumwa kutangaza na kushuhudia upendo wa huruma ya Mungu kwa watu wote wa Mataifa.

Makardinali hawa wakaingizwa kwenye Jimbo kuu la Roma ili kuonesha mahusiano na mafungamano kati ya Khalifa wa Mtakatifu Petro na Makanisa mahalia yaliyoenea sehemu mbalimbali za dunia.

Uteuzi na hatimaye, kusimikwa kwa Makardinali wapya ni changamoto kubwa inayowataka kujizatiti zaidi katika kutangaza na kushuhudia Injili ya Kristo Yesu, kwa kuhakikisha kwamba, imani inamwilishwa katika matendo; daima wakijielekeza zaidi katika huduma kwa watu wa Mungu sehemu mbalimbali za dunia.

Makardinali wanaojitambulisha kwa mavazi mekundu, wanaitwa kusadaka maisha yao kwa ajili ya Kristo Yesu na Kanisa lake, tayari kuwashirikisha watu wa Mataifa, ile furaha ya Injili.

Ni mwaliko wa huduma makini kwa watu wa Mungu. Jicho la kibaba linalooneshwa na Baba Mtakatifu Francisko kwa kutoa kipaumbele cha pekee kwa: Amani, mazingira, maskini na wale wote wanaosukimizwa pembezoni mwa jamii, ni chachu ya matumaini na mapendo ambayo yanapaswa kutawala katika maisha ya watu!

Makardinali waliosimikwa tarehe 30 Septemba 2023.

Baba Mtakatifu Francisko tarehe 13 Aprili 2023 alimteuwa Askofu mkuu Protase Rugambwa kuwa Askofu mkuu mwandamizi mwenye haki ya kurithi Jimbo kuu la Tabora, Tanzania na tarehe 9 Julai 2023 akamteuwa kuwa ni Kardinali wa tatu kutoka nchini Tanzania na kusimikwa rasmi tarehe 30 Septemba 2023.

Kardinali Protase Rugambwa, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Tabora akasimkwa rasmi tarehe 10 Novemba 2023 na hivyo kuchukua nafasi ya Askofu mkuu Mstaafu Paulo Runangaza Ruzoka wa Jimbo kuu la Tabora.

Ni katika muktadha huu, Kardinali Protase Rugambwa, “Kardinali Padre” Dominika tarehe 18 Februari 2024, anakabidhiwa Kanisa la “Santa Maria in Montesanto”, lililoko kwenye Barabara la Babuino, namba 198, Roma, kuashiria kwamba, Kardinali Rugambwa sasa ni sehemu ya Wakleri wa Roma, wanaounda Baraza la Makardinali lenye jukumu la kumsaidia Khalifa wa Mtakatifu Petro katika shughuli zake za kichungaji kama Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Roma.

Makardinali ni washauri wakuu wa Khalifa wa Mtakatifu Petro

Itakumbukwa kwamba, Kardinali Protase Rugambwa alizaliwa tarehe 31 Mei 1960 huko Bunena-Bukoba nchini Tanzania, akapata Daraja Takatifu ya Upadri kutoka mikononi mwa Mtakatifu Yohane wa Pili alipotembelea Tanzania tarehe 2 Septemba 1990 na kuwa Padri wa Jimbo Katoliki Rulenge-Ngara. Kuanzia mwaka 2002 hadi mwaka 2008 alifanya utume wake kwenye Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu mjini Vatican.

Baba Mtakatifu Benedikto XVI, tarehe 18 Januari 2008 akamteuwa kuwa Askofu wa Jimbo Katoliki Kigoma, na tarehe 26 Juni 2012 akateuliwa kuwa Katibu Mwambata wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa Watu na Rais wa Mashirika ya Kipapa ya Kimisionari na wakati huo huo kumpandisha hadhi na kuwa ni Askofu mkuu.

Tarehe 9 Novemba 2017 Baba Mtakatifu Francisko akamteuwa kuwa Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu.

Baada ya kulitumikia Baraza kwa vipindi viwili na muda wake ulipogota ukomo, kadiri ya Katiba mpya ya Kitume inayojulikana kama “Predicate evangelium” yaani “Hubirini Injili” Juu ya Sekretarieti kuu “Curia Romana” na Huduma Yake Kwa Kanisa na Kwa Ulimwengu”.

Tarehe 13 Aprili 2023, Baba Mtakatifu akamteuwa Askofu Mkuu Protase Rugambwa kuwa Askofu mkuu wenye haki ya kurithi Jimbo kuu la Tabora, Tanzania na hatimaye, kusimikwa rasmi kama Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Tabora tarehe 10 Novemba 2023.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live