Dini

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kanisa lakemea ushoga

Mtamya Askofu Ezra Enock

Mon, 16 Aug 2021 Chanzo: ippmedia.com

Kanisa la pentekoste motomoto PMC limeiomba serikali kuendelea kukemea na kukataa vitendo vya viashiria vyovyote vya mapenzi ya jinsia moja.

Kauli hiyo ilitolewa jana Agosti 15, na Askofu wa Kanisa hilo Tanzania, Ezra Enock, wakati wa harambee ya kuchangia ujenzi wa madarasa matatu ya Chuo cha Theolojia, mabweni pamoja na jengo la utawala katika makao makuu ya kanisa hilo, Boko jijini Dar es Salaam.

"Tunampongeza Rais Samia kwa jitihada mbalimbali anazoendelea kuzifanya katika kuliletea maendeleo taifa hili, tunaomba pia serikali iendelee kukemea na kukataa vitendo vya mmomonyoko wa maadili ikiwamo mapenzi ya jinsia moja, kwa sababu hii ni dhambi kubwa na inaweza kusababisha maafa kwenye taifa," alisema Askofu Enock.

Pia, Askofu Enock aliiomba serikali kukemea baadhi ya wanawake wanaovaa mavazi yasiyo na maadili.

"Na tunaiomba pia serikali kukemea na kuwadhibiti baadhi ya wanawake wanaovaa nguo za kikahaba kwa sababu vitendo hivi vinachangia kuharibu maadili mema kwenye Taifa letu," alisema Askofu Enock.

Kadhalika, Askofu Enock alimpongeza Rais Samia kwa kutoa kipaumbele  kwenye suala la kukuza uchumi wa nchi, kuimarisha ushirikiano wa kimataifa pamoja na kiziagiza mamlaka zinazohusika kupunguza mlundikano wa kesi mahakamani zisiso na ushahidi.

"Tunampongeza Rais Samia kwa kuona uchumi kuwa ndiyo kipaumbele chake cha kwanza na uchumi endelevu hujengwa palipo na misingi ya haki," alisema Askofu Enock na kuongeza:

"Tunaona miradi mbalimbali inaendelea kujengwa ikiwamo ile ya reli, miundombinu, miradi ya umeme, hiyo yote ni fursa pia za ajira, kwa hiyo tunampongeza sana Rais Samia."

Mbali na hilo, alisema kanisa hilo linampongeza Rais Samia kwa kufanya suala la chanjo ya ugonjwa wa virusi vya corona kuwa la hiari.

Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya Itikati na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi, Shaka Hamdu Shaka, alisema kutokana na mambo mbalimbali ambayo serikali inafanya, bado kidogo kipato cha kila Mtanzania mmoja mmoja kitaanza kuongezeka kwa kasi.

Hivyo, aliliomba kanisa hilo lisiunge mkono viashiria vyovyote vya uvunjifu wa amani nchini.  

"Rais Samia amenituma kwamba serikali itaendelea kuheshimu uhuru wa kuabudu na inatambua mchango wa kanisa katika maendeleo ya nchi," alisema Shaka na kuongeza.

"Ninaomba Watanzania waendelee kumuunga mkono Rais Samia, serikali yake inafanya mambo makubwa na baada ya muda mfupi mambo mazuri yanakuja, na kipato cha mtu mmoja mmoja kinakwenda kuongezeka."

Katika harambee hiyo Shaka alisema Rais Samia alichangia Sh.milioni 10, huku yeye akichangia Sh. milioni tano.

Chanzo: ippmedia.com