Australia. Jaji Mkuu nchini Australia, Peter Kidd amemhukumu kifungo cha miaka sita gerezani Kadinali George Pell baada ya kukutwa na hatia ya kuwanyanyasa kingono wavulana wawili.
Wavulana hao ni wale waliokuwa wakiimba kwaya katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Patrick, Melbourne zaidi ya miaka 20 iliyopita.
Jaji Kidd ameamuru leo Jumatano kuwa Kardinali Pell atumikie kifungo cha miaka mitatu na miezi minane gerezani kabla ya kustahili kupatiwa msamaha.
Pell ambaye pia alikuwa Waziri wa Uchumi wa Vatican, alikutwa na hatia Desemba mwaka jana kwa kumlawiti mvulana wa miaka 13 na kumdhalilisha kinyume cha maadili mvulana mwingine pia mwenye umri wa miaka 13 mwishoni mwa miaka ya 1990.
Matukio hayo yametokea miezi michache baada ya Pell kuteuliwa kuwa Askofu Mkuu wa Melbourne.