Mbulu. Waziri wa Katiba na Sheria Profesa Palamagamba Kabudi anatarajiwa kumwakilisha Rais John Magufuli katika ibada ya kusimikwa kwa Askofu mteule wa Jimbo Katoliki la Mbulu, Anthony Lagwen itakayofanyika kesho Jumapili Agosti 12, 2018.
Akizungumza na MCL Digital leo Jumamosi Agosti 11, 2018 mkuu wa Wilaya ya Mbulu, Chelestino Mofuga amesema wageni mbalimbali wameanza kuwasili Mbulu.
“Mgeni rasmi atakuwa Rais John Magufuli ambaye atawakilishwa na Profesa Kabudi,” amesema.
Amesema zaidi ya kupokea wageni amekagua maandalizi yote na ameridhika nayo, kubainisha kuwa ibada hiyo itafanyika katika kanisa Katoliki la Bikira eneo la Sanu mjini Mbulu.
Askofu mteule Anthony Lagwen alizaliwa Julai 5, 1967 katika kijiji cha Tlawi, wilayani Mbulu mkoani Manyara.