Dini

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

KKKT yalia utapeli makanisa ya kisasa

Isaack Kisiri Askofu Isaack Kisiri

Mon, 4 Sep 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Waumini wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), wametakiwa kujiepusha na makanisa yaliyoibuka hivi karibuni, yanayodaiwa kutoa mafundisho ya kitapeli kinyume na misingi ya dini ya kikristo. 

Wito huo umetolewa na Askofu wa KKKT Dayosisi ya Magharibi Kati (Tabora), Isaack Kisiri, akisoma neno la Mungu katika maadhimisho ya miaka 60 ya kanisa hilo, yaliyofanyika jijini Arusha na kuhudhuriwa na wageni mbalimbali wakiwemo wa dini nyingine na viongozi wa Serikali.

“Pamezuka mafundisho ya utapeli na wizi kwa kutumia jina la Yesu, utasikia watu wanaambiwa chukua simu yako zungusha na hela zitaingia, wengine huambiwa kutoa kiasi fulani cha fedha ili nyota zao zisafishwe na Baraka zao zilizochukuliwa na nguvu za giza zirejeshwe. Yale mambo ya kishirikan tunayopinga kanisani sasa yamekuwa sehemu ya ibada zetu,” amesema Askofu Kisiri.

Askofu Kisiri amedai kuwa, kuna baadhi ya makanisa yanawafundisha waumini wake kuwa wavivu katika kutafuta maisha.

“Tunaishi katika nyakati ambazo uvivu wa kiakili na kiroho umeshika kasi kubwa, wakristo wa sasa hawapendi mambo magumu, hawapendi kufanya kazi badala yake wameweka imani katika vitu, chumvi ya upako, maji ya upako na sasa kuna kaptula ya upako.

"Wanategemea mambo haya wafanikishe kiuchumi na kimaisha badala ya kufanya kazi kwa bidii na kuweka imani kwa Yesu ambaye ni siri ya mafanikio kiroho na kimwili,” amesema Askofu Kisiri.

Kiongozi huyo wa dini, ametoa tahadhari hiyo wakati akielezea mafanikio na changamoto za KKKT ilizopitia katika kipindi cha miaka 60.

Akitaja mafanikio ya KKKT ndani ya miaka 60, Askofu Kisiri amesema idadi ya dayosisi zimeongezeka kutoka saba hadi 27, huku nyingine zikiwa mbioni kuanzishwa. Idadi ya waumini imeongezeka kutoka 500,000 hadi kufikia 8,000,000.

“Tulianza tukiwa tunachechemea tunaomba msaada, tunatembeza bakuli, leo tunasimama kwa miguu yetu wenyewe tumeshika kazi ya Mungu,” amesema Askofu Kisiri.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live