Arusha. Wafanyakazi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC)na viongozi wa madhehebu ya dini wameshiriki ibada maalumu ya kuombea watu waliofariki katika ajali ya kivuko cha Mv Nyerere iliyotokea Septemba 20 mwaka huu.
Akizungumza leo Jumanne, Septemba 25 baada ya maombi hayo yaliyofanyika katika makao makuu ya jumuiya hiyo, katibu mkuu wa jumuiya hiyo ,Libearat Mfukukeko amesema wamepokea kwa mshtuko taarifa za msiba huo uliosababisha vifo zaidi ya watu zaidi ya 200 kwani Taifa limepoteza nguvu kazi kubwa.
Hata hivyo, katibu mkuu alitoa salamu za rambirambi kwa Rais John Magufuli kuwataka makatibu wakuu waliokutana Septemba 6 mwaka huu kwa ajili ya kuunda kituo maalumu cha uokozi kufanya haraka ili kuanzisha kituo cha uokozi ili kiweze kutoa msaada pindi yanapotokea majanga mbalimbali ya aina hii.
Kwa upande wake Spika wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Martin Ngoga ameungana na Watanzania katika majonzi kwa kushiriki ibada hiyo, huku akizitaka serikali za jumuiya hiyo kuhakikisha zinachukua hatua dhabiti za kuhakikisha majanga kama hayo hayajirudii katika eneo la Ziwa Victoria.
Mwenyekiti wa Bunge la Afrika Mashariki ,Dk Abdallah Makame amesema kutokana na sheria ya usafiri wa Ziwa Victoria iliyotaka kuanzishwa kwa kituo cha uokoaji na kutiwa saini Mei 2008 na maraisi kama ingefanyiwa kazi kipindi hicho ingeweza kusaidia kuokoa zaidi ya watu waliochukua muda mrefu kupatiwa msaada.