Kisarawe. Pacha waliotenganishwa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) Dar es Salaam nchini Tanzania, Gracious Mkono (Nyamiri) na Precious Mkono (Telya) wamekabidhiwa nyumba ikiwa ni miezi 10 tangu benki ya UBA iwaahidi.
Pacha hao waliozaliwa Kisarawe mkoani Pwani nchini Tanzania, Julai 12, 2019 na kufanyiwa upasuaji Septemba 23, 2018 wamekabidhiwa nyumba hiyo leo Jumanne Septemba 24, 2019 na Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe mkoani humo, Jokate Mwegelo.
Akizungumza wakati wa kukabidhi nyumba hiyo, Mwegelo amesema haikuwa rahisi kukamilisha ujenzi huo kutokana na migogoro iliyokuwepo katika familia hiyo.
“Wengi wanaweza kushangaa kwa nini imechukua muda mrefu kukamilika, lakini kulikuwa na migogoro ya familia, ilibidi tukae na wazee wa kimila kuwaeleweshe na baada ya makubaliano walisaini hati kama ushahidi na ujenzi ulianza mara moja,” amesema.
Amesema nyumba hiyo iliyojengwa Mzenga, ipo karibu na huduma muhimu ikiwemo shule, barabara, hospitali, umeme, maji, barabara na imechukua siku 28 kukamilika.
Mkurugenzi Mkuu wa United Bank for Africa (UBA) Usam Isihaka amesema licha ya kukabidhi nyumba hiyo UBA iliahidi kuhakikisha watoto hao wanapatiwa bima ya afya ya miaka kumi pamoja na kuwafungulia akaunti yenye akiba ya Sh2 milioni ambayo tayari imefunguliwa.
Pia Soma
- Boris ashangazwa wakurugenzi Thomas Cook kulipwa mamilioni
- DC Dodoma atangaza operesheni kuwasaka vibaka
- Simba, Nyati wapagawisha washiriki tamasha la Jamafest
- Tanzania kupewa uenyeji Jamafest 2032
Awali, Februari 9 2019 Mwananchi ilifanya ziara kuona hali ya watoto hao wanaoishi katika kitongoji cha Kigogo kilichopo kijiji cha Kimara Misale, wilaya ya Kisarawe ikiwa ni umbali wa kilomita 35 kutoka Ruvu - Vigwaza barabara ya Morogoro na kuwakuta wakiwa bado hawajakamilishiwa ahadi hiyo.