Arumeru. Mkuu wa Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro, Lengai ole Sabaya, amewaomba viongozi wa dini nchini kutohubiri neno la Mungu kwa njia ya mapokeo yasiyo na faida kwa waumini kwani hakuna Serikali inayopingana na viongozi wa dini.
Sabaya ameyasema hayo leo Jumatatu Mei 27, 2019 kwenye mazishi ya mmiliki wa mgodi wa vito vya Tanzanite, Thomas Mollel maarufu askofu yaliyofanyika kata ya Mbuguni wilayani Arumeru mkoani Arusha.
Sabaya amesema hakuna Serikali inayopingana na viongozi wa dini ila wanapaswa kuongozwa na roho mtakatifu wanapotoa mahubiri yao.
Amesema viongozi wa dini wanapaswa kutoa maneno ya faraja kwa viongozi vijana sio kuwaita majina ya ajabu ikiwamo kifutu.
"Viongozi wa dini tunawaheshimu kwani hakuna Serikali yoyote inayopingana nao ila sio vizuri kuwaita majina ya ajabu ajabu viongozi wa Serikali," amesema.
Amesema viongozi wa dini hawapaswi kuhubiri mapokeo yasiyo na maana kwa waumini ikiwamo kuilaumu kuwa hivi sasa sadaka imepungua sababu ya Serikali.
Pia Soma
- MADAI: DPP awatuhumu wabunge kwa rushwa, Spika ajibu
- Ajiua baada ya kumuua mkewe, mama mkwe na jirani kwa wivu wa mapenzi
- Mbunge ahoji ziko wapi Noah za Watanzania
Murro amesema wao kama Serikali pamoja na kutoa pole wanawaomba wananchi wa eneo hilo waendeleze yale mema yote yaliyofanywa na Mollel.
"Hakuwa na tatizo na mtu, amefanya maendeleo mengi akiwa diwani kwa kujenga zahanati, kuboresha kituo cha afya sisi tuliokuja badala yake tunaweka alama gani?" amehoji Murro.
Amesema kielelezo tosha kwa marehemu ni ndugu wa kusimama imara na wasigombane kwa sababu ya mali.
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Arusha, Loota Sanare alimshukuru aliyekuwa mbunge wa Jimbo la Arumeru Mashariki, Joshua Nasari (Chadema) kuhudhuria mazishi hayo.
Katibu wa UVCCM, Raymond Mwangwala amesema Askofu alikuwa na upendo uliopitiliza ndio sababu aliwahi kurusha fedha kwa wanachi akiwa kwenye hoteli yake ya Pallsons jijini Arusha.
Amesema Mollel hakuwa mbinafsi ndio sababu akawa na upendo ili watu wote wapate kutokana na upendo mkubwa aliokuwa nao.