Dar/mikoani. Ushiriki wa baadhi ya waumini katika makanisa mbalimbali nchini jana haukuwa ule uliozoeleka baada ya kuchukua tahadhari dhidi ya maambukizi ya virusi vya corona.
Miongoni mwa mabadiliko hayo ni idadi ya waumini kupungua ukilinganisha na kawaida, idadi ya misa kuongezwa ili kupunguza wingi wa watu kanisani na utaratibu wa kupokea sakramenti kubadilika.
Pia, hayakuwapo maji ya baraka katika milango ya kuingia makanisani ambayo waumini huchovya mikono yao.
Mwananchi lilishuhudia baadhi ya makanisa waumini wakinawa mikono kwa maji na sabuni na mengine wakipaka vitakasa mikono (sanitizer).
Hadi kufikia jioni, ugonjwa huo ulikuwa umesambaa katika nchi 188 kati ya 195 duniani, watu 316,792 wakiambukizwa, kati yao 13,573 wakifariki dunia. Watu zaidi ya 96,000 wamepona maambukizi hayo.
Kwa mujibu wa barua ya Katibu Mkuu Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Brayton Kilewa iliyosomwa jana katika ibada wilayani Moshi, mbali na kusisitiza elimu, pia imeelekeza kusitisha ibada kwenye jumuiya, mafundisho ya kipaimara, mikutano, makongamano, matamasha na semina zote zisizokuwa za lazima, hadi hapo watakapotangaziwa.
Habari zinazohusiana na hii
- VIDEO: Mgonjwa wa kwanza nchini kuugua corona apona
- Corona inavyogeuka ‘janga’ la uchaguzi kwa baadhi ya nchi
- VIDEO: Wagonjwa wa corona Tanzania wafikia 12, wasafiri kuwekwa karantini siku 14 kwa gharama zao
- VIDEO: Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro atia neno mapambano dhidi ya corona
Katika ibada mjini Dodoma, Padri Onesmo Uwiso kupitia kwa muumini James Jonas alisema Kanisa Katoliki jijini humo limeongeza idadi ya misa kwa siku kutoka nne hadi sita ili kupunguza msongamano kanisani kwa lengo la kujikinga na ugonjwa wa corona.
Pia, katika Parokia ya Kiwanja cha Ndege, Dodoma, waumini walielekezwa kunawa maji yaliyowekwa kemikali katika ndoo katika milango yote ya kuingilia kanisani.
Ndoo nyingine ziliwekwa katika geti la kanisa na waliosimamia ibada walikuwa wakiwaelekeza waumini kunawa mikono kabla ya kuingia kanisani.
Milangoni hakukuwa na maji ya baraka na wakati wa misa hakukuwa na kipengelea cha kutakiana amani kwa kupeana mikono kama ilivyo kawaida.
Jijini Dar es Salaam katika makanisa ya Mtakatifu Peter, Kanisa Katoliki la Mtakatifu, Azania Front, Mtakatifu Albani na Kanisa la Ufufuo na Uzima nako hadhari ilionekana kuchukuliwa.
Katika ibada za kwenye makanisa hayo, waumini walinawa mikono katika maji ya sabuni na wenye utaratibu wa kuchovya maji ya baraka hawakufanya hivyo.
Utamaduni mwingine ulioonekana kubadilika katika makanisa kadhaa ni kusalimiana kwa ishara badala ya kupeana mikono.
ikiwemo