Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata), limesema Sikukuu ya Eid el Adh’haa itakuwa Jumatatu Juni 17 na swala yake itaswaliwa katika msikiti wa Mohamed VI uliopo makao makuu ya baraza hilo Kinondoni.
Taarifa iliyotolewa leo Jumamosi Juni 8, 2024 na Katibu Mkuu wa Bakwata, Alhaji Nuhu Mruma swala ya Eid itaanza saa moja asubuhi ikifuatiwa na Baraza la Eid litakalofanyika pia katika msikiti huo.
“Kwa niaba ya Bakwata, Mufti na Sheikh mkuu wa Tanzania, Abubakar Zubeir anawatakia maandalizi mema ya sikukuu hiyo,” amesema Alhaj Mruma katika taarifa hiyo.
Eid El Adh’haa ni sikukuu inayoadhimishwa baada ya waumini wa Kiislamu kukamilisha ibada ya Hijja ambayo ni nguzo ya tano katika nguzo za dini.
Nguzo ya kwanza ni shahada ambayo Muislamu anapaswa atoe shahada kwa kusema: Nakiri kuwa hakuna Mungu isipokuwa Allah na kwamba Muhammad ni mjumbe wa Allah.
Nguzo ya pili ni kuswali swala tano zilizowekewa nyakati maalumu kuanzia, alfajiri hadi usiku. Swala hizo ni Fajr (huswaliwa alfajiri), Dhuhr (huswaliwa mchana adhuhuri), Laasir (huswaliwa alasiri, Maghrib (huswaliwa baada ya jua kuzama) na Ishai (huswaliwa usiku unapoingia hadi karibu na alfajir).
Eid el-Adha maana yake ni ‘sikukuu ya kutoa kafara/kuchinja’ na hutumiwa kukumbuka tukio la Nabii Ibrahimu alipotaka kumtoa kafara mwanawe Ismael.
Allah Mtukufu alimwamuru Nabii Ibrahim kumchinja mwanawe akimpima imani, wakati Nabii Ibrahim akiwa tayari kutekeleza amri hiyo, Allah Karimu akamshushia kondoo kama kafara badala ya mwanawe huyo wa kwanza.