Butiama. Askofu wa Jimbo Katoliki la Musoma mmoani Mara nchini Tanzania, Michael Msonganzila amefichua siri ya Mkuu wa Majeshi mstaafu, Jenerali David Msuguri kuishi miaka 100 ya kuzaliwa.
Akihubiri wakati wa misa takatifu ya shukrani nyumbani kwa Jenerali Msuguri kijiji cha Butiama mkoani Mara leo Jumamosi Januari 4, 2020, Askofu Msonganzila ametaja mazoezi ya kijeshi, nidhamu ya maisha na vyakula vya asili kuwa miongoni mwa siri za mkuu huyo wa majeshi kuishi miaka mingi.
"Hofu ya Mungu ni siri nyingine iliyomfanya Mzee Msuguri kuishi miaka mingi," amesema Askofu Msonganzila
Amesema maisha ya amani na heshima kuanzia ndani ya familia, serikalini na jamii kwa ujumla pia ni miongoni mwa sababu za Jenerali Msuguri kuishi miaka 100.
Huku akianza mahubiri yake kwa kuongoza familia, ndugu, jamaa, marafiki na viongozi kadhaa wa Serikali na kijamii kumwimba wimbo wa "happy birthday" Askofu Msonganzila amemwombea Jenerali Msuguri kuishi miaka mingine 100 na kufikisha miaka 200.
Jenerali Msuguri aliyezaliwa Januari 4, 1920 leo anatimiza miaka 100.
Akiwa mkuu wa majeshi, yeye ndiye aliongoza vikosi vya Tanzania kumpiga aliyekuwa Rais wa Uganda, Idd Amin Dada katika vita ya Kagera mwaka 1979.
Idd Amin alivamia eneo la Kagera na kushusha bendera za Tanzania na kupandisha za Uganda hali ambayo ilichukizwa na Rais wa Tanzania wa wakati huo Hayati Mwalimu Julius Nyerere na kutangaza vita ambayo Tanzania ilishinda chini ya Jenerali Msuguri