ASKOFU Mkuu wa Kanisa la Tanzania Assemblies of God (TAG), Dk Barnabas Mtokambali amewataka waumini wa kanisa hilo kuliombea taifa ili Mungu alivushe salama na kufanyika faraja, amani na utulivu kwa watanzania wote.
Dk Mtokambali alisema hayo katika salamu za rambirambi za kanisa hilo alizozitoa kwa taifa katika kipindi hiki cha kuondokewa na Rais wa Awamu ya Tano, John Magufuli anayetarajiwa kuzikwa kesho.
Alilitaka kanisa hilo kushiriki kikamilifu katika kipindi hiki cha maombelezo kwa kadiri serikali itakavyotoa maelekezo.
"Kwa hakika huu ni msiba mkubwa kwa taifa letu kwa kuondokewa na kiongozi mkuu wa nchi aliyeko madarakani. Tunamuomba Mungu atupe neema ya kuvuka salama. Hivyo basi tunawaomba washirika wote wa TAG na watanzania wote kwa ujumla kuendelea kudumisha umoja, amani na mshikamano wa nchi,"alisema.
Dk Mtokambali pia alitaka Wakristo kuheshimu mwongozo na maelekezo yaliyopo kwenye Katiba, Ibara ya 37 (5) kuhusiana na tukio hilo lililoipata nchi.
Aliwataka wakristo kuliombea taifa dhidi ya maadui wa nje na ndani katika kipindi hiki wasitumie mwanya wowote kuihujumu nchi.
Ikiwa ni pamoja na kuviombea vyombo vya ulinzi na usalama katika kusimamia na kudumisha amani, utulivu na mshikamano wa taifa.
"Tunatoa pole nyingi kwa Mama Janeth Magufuli, pia tunatoa pole nyingi kwa Rais Samia Suluhu Hassan pamoja na watanzania wote kwa msiba huu mkubwa ulilolipata taifa letu. Mungu wa faraja zote, atufariji sote," alisema.