Dar es Salaam. Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Mashariki na Pwani, Alex Malasusa amewahimiza wananchi kumtanguliza Mungu kwa kila jambo wanalolifanya ikiwamo shughuli za kujiletea maendeleo.
Askofu Malasusa ametoa kauli leo Jumatano Januari Mosi, 2020 wakati akiendesha ibara ya kusherekea mwaka mpya iliyofanyika katika kanisa la Azania Front Dar es Salaam.
"Hatuna sababu ya kukaa kimya, hii ni neema ya Mungu. Huu ni mwaka wa ibada watu wasikae nyumbani wahimizwe kwenda kwenye nyumba za ibada, pia tumtangulize Mungu kwa kila jambo na tumshukuru kwa mema katika mwaka uliopita," amesema Askofu Malasusa.
Amesisitiza ujumbe mkubwa kwa kanisa hilo katika kusherekea mwaka mpya ni kuwakumbusha wananchi kumtegemea na kuomba Mungu kila wakati na siku zote na kufanya matendo yanayompendeza.
Askofu huyo amewatakia pia wananchi heri ya mwaka mpya wenye baraka, furaha na amani huku akiwataka kufanya kazi kwa bidii kwa ajili ya kujiletea maendeleo.
Kuhusu uchaguzi mkuu wa mwaka 2020, Askofu Malasusa amesema siku zote viongozi wa dini wamekuwa wakiombea chaguzi zenye amani, zisizo na vurugu zitakazoleta viongozi bora.
"Hawa wanaongoza wameumbwa na Mungu ambaye amewachagua ili watu wake waongozwe kwa mema," amesema Askofu Malasusa.