Arusha. Familia ya kijana, Nelson Olutu ambaye alifariki katika ajali ya ndege jana, imeelezwa leo Jumanne alikuwa anahitimu rasmi mafunzo ya urubani kwa vitendo.
Orutu akiwa na rubani wa ndege ya Kampuni ya Auric Air, Nelson Mabeyo walifikwa na mauti jana Jumatatu Septemba 23, 2019 katika uwanja wa ndege wa Soronera ndani ya Hifadhi ya Serengeti nchini Tanzania.
Orutu alikua akisoma katika Chuo cha Urubani cha Nairobi Huston Airport (Proactive Aviation) alikua katika likizo ya mafunzo kwa vitendo ambapo alikuwa akifanya safari za kujifunza kuendesha ndege na hadi anapata ajali alikuwa amebakiza saa 30 kutimiza mafunzo.
Wawili hao walifariki katika ndege hiyo iliyokuwa ikiruka kwenda eneo la Grumeti ndani ya hifadhi hiyo kuchukua watalii kuwapeleka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa Kilimanjaro (KIA) nchini Tanzania.
Akizungumza na Mwananchi akiwa msibani eneo la kwa Mrefu nje kidogo ya Jiji la Arusha leo Jumanne Septemba 24, 2019, Kaka wa Marehemu Kelvin Orutu amesema familia imepokea kwa mshtuko mkubwa msiba huo.
Habari zinazohusiana na hii
- Ndege yaanguka hifadhi ya Serengeti Tanzania, yaua wawili
- VIDEO: Mtoto wa Mabeyo aliyekufa kwenye ajali ya ndege alitarajia kuajiriwa ATCL
- VIDEO: JWTZ waanza uchunguzi ajali ya ndege iliyoua mtoto wa CDF Mabeyo
- Mtoto wa mkuu wa majeshi Tanzania afariki ajali ya ndege
Kelvin amesema alikuwa ofisini wakati akipokea taarifa za msiba wa mdogo wake kutoka kwa mfanyakazi mwenzake ambaye alimweleza mdogo wake amepata ajali.
"Aniambia asee mdogo wako Nelson amepata ajali na yuko hospitali anaendelea vizuri, ila niliweza kutambua kuna tatizo kubwa na ananifisha ukweli ndipo niliamua kuwatafuta rafiki zake ambao walinipa taarifa za msiba," amesema
Amesema Nelson aliondoka siku ya Jumapili nyumbani na aliieleza familia anakwenda na rafiki yake, Nelson Serengeti kwa ajili ya kubeba watalii na ndipo walipopata ajali.
Imendikwa na Mussa Juma, Mohamed Kaoneka na Noel Macha, Mwananchi