Katibu Tawala Mkoa wa Mbeya, Dk. Angelina Lutambi ameyasema hayo mkoani humo kwenye maadhimisho ya siku ya Mtoto wa Afrika ambayo yalifanyika kimkoa katika kijiji cha Ipinda wilayani Kyela.
Amesema watoto waliofanyiwa ukatili huo ni kuanzia miaka sifuri hadi 14 na kwamba idadi ya watoto 196 walifanyiwa ukatili wa kingono, wa kimwili 222, kihisia 296 wa kutelekezwa 84.
“Takwimu hizi ndugu zangu ni mbaya, zinaonyesha ni jinsi gani jamii haiwajibiki na haizingatia sheria katika kuwajibika kumlinda mtoto na vitendo vya unyanyasaji wa watoto huanzia ngazi ya familia, yatupasa kubadilika na kuongeza umakini katika malezi ya watoto muhimu wanandoa kudumisha amani na upendo ili kuepusha madhara kwa watoto,” amesema Dk. Lutambi.
Ameongeza kuwa madhara yanayoweza kujitokeza endapo wazazi hawatakuwa na malezi bora kwa watoto ni kuwa na idadi kubwa ya watoto yatima, wanaoishi katika mazingira magumu ambao wengi wao huishia kuwa ombaomba mitaani na kujiingiza kwenye vitendo vya uhalifu, pamoja na kuongezeka kwa maambukizi ya virusi vya ukimwi.