WANAFUNZI zaidi ya 3,000 waliomaliza darasa la saba na kuchaguliwa kujiunga na masomo ya sekondari mwaka 2021 wamekosa nafasi kutoka na ukosefu wa vyumba vya madarasa Mkoani Kilimanjaro.
Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mgwhira aliyasema hayo leo wakati akizungumza na watendaji wa halmashauri, katika kikao maalumu cha kujadili mstakabali wa kutatua changamoto ya uhaba wa madarasa.
Mghwira alisema Mkoa wa Kilimanjaro katika wilaya za Hai, Moshi Vijijini, Same na Siha unakabiliwa na uhaba wa Madarasa zaidi ya 60 ambapo changamoto hiyo imesababisha wanafunzi hao kukosa nafasi ya kuendelea na kidato Cha kwanza.
"Katika Mwaka 2021 wa masomo wanafunzi 2900 hawataweza kuendelea na kidato Cha kwanza kutokana na uhaba wa madarasa, ambapo wilaya ya Hai Ni wanafunzi 890, Moshi vijijini 350, Same 1,414 na Siha 350," alisema.
Aidha alisema katika wilaya ya Hai inakabiliwa na uhaba wa madarasa 18, Moshi Vijijini saba, Same 28 na Siha saba na kwamba halmashauri peke ambazo hazijakabiliwa na changamoto hizo ni pamoja na Moshi manispaa, Rombo na Mwanga.