Arusha. Halmashauri ya wilaya ya Longido mkoani Arusha imeweka vipaumbele miradi ya kimkakati itakayoongeza mapato kufikia Sh22 bilioni katika kipindi cha miaka mitatu ijayo.
Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri hiyo, Jumaa Mhina amesema hayo leo Ijumaa Desemba 28, 2018 katika mkutano na waandishi wa habari wakati akieleza mafanikio ya uongozi wa awamu ya tano pamoja na miradi iliyofanywa.
Ameitaja miradi hiyo ni uegeshaji wa malori, ufugaji wa nyuki, ushuru kutoka kiwanda cha nyama, dampo la kisasa na kituo cha mabasi.
"Mikakati hii tuliyoiweka na kasi ya Rais John Magufuli ambayo ameionyesha, tunaamini wilaya yetu itakua kati ya halmashauri zenye kutoa mchango muhimu kiuchumi na kijamii," amesema Mhina.
Mkuu wa wilaya hiyo, Frank Mwaisumbe amesema katika kipindi cha miaka mitatu ya uongozi wa Rais Magufuli wilaya hiyo imepokea kiasi cha Sh41 bilioni kwa ajili ya shughuli mbalimbali za maendeleo.
Amepongeza ununuzi wa ndege ambao utachochea kuongezeka kwa idadi ya watalii watakaotembelea vivutio nchini.