Tabora. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kesho anatarajia kuanza ziara ya siku tatu mkoani Tabora kwa kutembelea wilaya za Igunga, Nzega na Tabora.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Tabora leo Agosti 15, mkuu wa mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri amesema ziara ya kiongozi huyo itaanzia wilayani Igunga ambapo atawasili asubuhi na kupokea taarifa ya utekelezaji ya mkoa kabla ya kuzungumza na viongozi, watendaji na watumishi wa halmashauri ya wilaya hiyo.
“Akiwa Igunga, Waziri Mkuu atatembelea kiwanda cha Manonga na kuhutubia mkutano wa hadhara,” amesema Mwanri.
Amesema Ijumaa Waziri Mkuu atatembelea wilaya ya Nzega ambako pia atazungumza na viongozi, watendaji na watumishi kabla ya kuhutubia mkutano wa hadhara mjini Nzega.
Majaliwa atahitimisha ziara yake Jumamosi kwa kutembelea Manispaa ya Tabora ambako atatembelea na kuona utendaji na huduma katika Hospitali ya Rufaa ya mkoa ya Kitete kabla ya kuhutubia mkutano wa hadhara katika uwanja wa Chipukizi mjini Tabora.
Hii ni mara ya pili Waziri Mkuu kutembelea mkoa wa Tabora mwaka huu baada ya ziara ya awali alipotembelea wilaya zinazolima zao la tumbaku za Sikonge, Uyui, Urambo na Kaliua.