Watu wawili wamenusurika kifo katika ajali iliyohusisha magari matatu, mawili yakiwa ni malori ya mizigo na moja likiwa gari dogo aina ya land cruiser.
Ajali hiyo iliyohusisha gari moja la mizigo kuteketea moto imetokea katika eneo la Seminari Manispaa ya Morogoro barabara kuu ya Morogoro - Dar es Salaam.
Kamanda wa jeshi la Zimamoto na uokoaji Goodluck Zelote amesema ajali hiyo imetokea majira ya saa tatu usiku wa kuamkia julai 16 mwaka huu chanzo cha ajali hiyo kikitajwa ni uzembe wa dereva wa lori lililokua linatokea Morogoro kugonga gari jingine kwa nyuma kisha kuwaka moto.
Kamanda Zelote amesema katika ajali hiyo hakuna vifo na mali zilizokua kwenye gari hilo liliteketea kwa moto.
Amesema majeruhi hao wameokolewa na wamekimbizwa hospitali ya Rufaa Mkoa Morogoro kwa matibabu zaidi.