Dar es Salaam. Leo Jumamosi Juni Mosi, 2019 ndio mwanzo wa matumizi ya mifuko mbadala baada ya nchi kuachana na matumizi ya mifuko ya plastiki lakini baadhi ya wafanyabiashara wa nyama jijini Dar es Salaam wamelalamikia matumizi ya mifuko hiyo kwa maelezo kuwa si rafiki kwa kufungia kitoweo hicho, bei yake ni kubwa.
Wakizungumza na Mwananchi leo, Shabani Ramadhani muuza nyama soko la Mapinduzi lililopo Mwananyamala amesema mifuko mbadala haifai kumfungia nyama mteja, wanalazimika kuwafungia kwenye magazeti.
"Mifuko tuliyoletewa haifai kufungia nyama ukiweka maini au utumbo ambao kwa kawaida una majimaji yanachuruzika chini hivyo," ameeleza Shabani.
Kuhusu bei, amesema mifuko mbadala huuzwa Sh300 hadi 350 hivyo mteja asipokuwa na fedha ya kununua mfuko huo wanalazimika kumfungia kwenye gazeti.
"Kitendo cha hii mifuko kuuzwa bei ya juu kidogo kinaweza kusababisha kupanda kwa bei ya nyama. Mteja hawezi kuja ukamuuzia nyama robo kilo ukampa na mfuko wa Sh300,” amesema Shabani.
George Mwakatobe, muuza nyama katika soko hilo amesema tatizo linalowakabili sasa ni uhaba wa mifuko mbadala.
Pia Soma
- Walichokisema wafanyabiashara wadogo Dar matumizi mifuko mbadala
- Kishindo cha kumalizika kwa tamthilia ya Sultan
- SIMULIZI ZA MUZIKI: Leo nimeukumbuka wimbo Sogea Karibu utunzi wa Belesa Kakere
Angel Joseph, mkazi wa Mwananyamala aliyekutwa na Mwananchi akinunua bidhaa mbalimbali sokoni hapo amesema wanapata tabu wanapokwenda kwenye mabucha kwa kuwa wanafungiwa nyama kwenye magazeti.
“Ukifungiwa nyama kwenye gazeti wakati mwingine nyama inabaki na rangi ya gazeti au wakati mwingine ukaipika na kipande cha gazeti,” amesema.