Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Watumishi wa mahakama mpya za wilaya wapigwa msasa

Watumishi Wa Mahakama Mpya Za Wilaya Wapigwa Msasa Watumishi wa mahakama mpya za wilaya wapigwa msasa

Wed, 30 Nov 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Watumishi wa Mahakama mpya za Wilaya 18 zilizozinduliwa hivi karibuni wanaendelea kupatiwa mada mbalimbali za kuboresha utendaji kazi wao katika Mafunzo yanayoendelea kutolewa kwenye Ukumbi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Morogoro.

Ikiwa ni siku ya pili ya mafunzo hayo, jana tarehe 29 Novemba, 2022 mada zilizotolewa ni pamoja na; Wajibu na Majukumu ya Mahakama za Wilaya, Utunzaji na matumizi sahihi ya Kumbukumbu na matumizi ya ofisi mtandao ‘e-office’, Mradi wa Uboreshaji wa Huduma za Mahakama.

Akiwasilisha Mada ya Wajibu na Majukumu ya Mahakama ya Wilaya, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sharmillah Sarwatt amewataka Watumishi wa Mahakama hizo kuwathamini wananchi ambao ndio wateja wanaosababisha wao kuwa kazi, hivyo huduma zitakazotolewa ziwe za viwango.

“Nadhani hapa wote mnafahamu majukumu ya Mahakama mnazofanyia kazi, hivyo tuko hapa kwa ajili ya kukumbushana ili kutoa huduma bora zaidi, ni matumaini yangu na Mahakama kwa ujumla kuwa mtaboreshaji utendaji kazi wenu kwa kufanya kazi kwa bidii ili kutimiza jukumu kuu la Mahakama la kutoa haki,” amesema Mhe. Sarwatt.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Nyaraka na Kumbukumbu- Mahakama ya Tanzania, Bw. Malimo Manyambula amewaasa Watumishi hao kuzingatia utunzaji sahihi wa nyaraka mbalimbali za ofisi na kuwaasa kutunza siri za ofisi na za wateja.

Akiwasilisha mada ya Mradi wa Uboreshaji wa Huduma za Mahakama, naye Mchumi Mwandamizi kutoka Kitengo cha Maboresho cha Mahakama ya Tanzania, Bi. Felister Fatukubonye amewaeleza washiriki wa Mafunzo hayo kuwa Mahakama ya Tanzania inatekeleza Mpango Mkakati wake wa mwaka 2020/2021-2024-2025, ambapo amewaeleza Watumishi hao kuwa Mahakama ya Tanzania bado inaendelea na uboreshaji wa huduma mbalimbali zenye lengo la kuhakikisha kuwa huduma ya utoaji haki inamfikia mwananchi kwa urahisi.

Aidha, Bi. Felister amesema kuwa, ili jitihada za Mahakama, Serikali na Wafadhili ziweze kuzaa matunda kunahitajika ushirikiano wa pamoja ikiwemo watumishi kubadili mtazamo na fikra ili uboreshaji za miundombinu na kadhalika viweze kwenda sambamba na utoaji huduma bora kwa wananchi.

Mafunzo haya ya Huduma kwa mteja yanaendelea kutolewa na Watumishi hao mpaka tarehe 02 Desemba, 2022 na mada nyingine zitatolewa ikiwemo Jinsi ya kukabiliana na msongo (Stress Management) na kadhalika.

Tarehe 25 Novemba, 2022 Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma alizindua Mahakama ya Wilaya Busega iliyowakilisha Mahakama nyingine mpya za Wilaya mpya 17, Mahakama hizo zilizojengwa kwa ufadhili wa Benki ya Dunia ni pamoja na; Butiama, Rorya, Songwe, Gairo, Mkinga, Mvomero, Kilombero, Mbogwe, Nyang’hwale, Kyerwa, Itilima, Missenyi, Kaliua, Uvinza, Buhingwe, Kakonko na Tanganyika.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live